29 Feb 2016


NEEMA YA WALIMU YAANZIA DAR- ES-SALAAM: KUSAFIRI BILA NAULI
 
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda akieleza jambo kuhusu mpango wa kusafirisha walimu wa shule za Serikali za Dar es Salaam bila ya kulipa nauli kwenye daladala. Kushoto ni Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Daladala (DARCOBOA), Sabri Mabrouk na Mwenyekiti wa Chama cha Madereva wa Daladala (Uwadar), William Masanja. Picha na Omar Fungo
Pengine hii yaweza kuwa ni historia; kuanzia Machi 7 walimu wa Mkoa wa Dar es Salaam wanaofundisha shule za Serikali za msingi na sekondari, hawatalipa nauli kwenye kwenye daladala wakati wakienda na kutoka kazini.
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda alitangaza hayo jana mbele ya viongozi wa vyama vya usafirishaji abiria na madereva Mkoa wa Dar es Salaam.
Makonda alisema wazo lake la kutaka walimu wasafiri bure limeungwa mkono na viongozi wa vyama vya wasafirishaji abiria na wamiliki wa daladala na kwamba kilichobaki ni kuanza kutoa huduma hiyo.
“Awali, wazo langu ilikuwa walimu wa Wilaya ya Kinondoni ninayoiongoza, ndiyo wafanyiwe utaratibu wa kusafiri bure lakini wadau wa usafirishaji wakashauri iwe kwa mkoa mzima. Nikamweleza mkuu wa mkoa na akaniruhusu tufanye hivyo mkoa mzima,” alisema Makonda ambaye mpango wake wa kuchangia ujenzi wa shule umemhakikishia cheo baada ya Rais John Magufuli kuguswa.
Makonda alisema kuanzia leo, wakuu wa shule za msingi watakakiwa kuwatengenezea walimu wao vitambulisho kwa ajili ya usafiri.
Mambo manne
Alisema vitambulisho hivyo ambavyo vitavaliwa wakati wa kupanda daladala, vitatakiwa kuwa na picha ya mwalimu, jina lake kamili na jina la shule anayofundisha.
Mkuu wa wilaya hiyo alisema vitu vingine vinavyotakiwa kuwa kwenye vitambulisho hivyo ni saini ya Makonda ili kuepuka udanganyifu na namba ya simu ya mkuu wa shule husika.
Alisema baada ya vitambulisho kukamilika, walimu watapanda bure katika daladala lolote wakati wa kwenda kazini kuanzia saa 11.30 hadi saa 2.00 asubuhi na kwamba wakati wanarejea nyumbani huduma hiyo itaanza saa 9.00 alasiri hadi saa 11.00 jioni.
Makonda alisema huduma hiyo ya usafiri bure kwa walimu itatolewa siku tano kwa wiki kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa na kwamba siku za Jumamosi, Jumapili na sikukuu watatakiwa kulipia.
“Huo ni muda ambao wamiliki wamekubali kusafirisha walimu bure kwenda kazini na kurudi nyumbani. Nje ya muda huo walimu watatakiwa kulipa nauli kama kawaida,” alisema.
Makonda alisema baada ya Rais Magufuli kutangaza elimu bure, aliona amuunge mkono kwa kuweka mazingira yatakayorahisisha utendaji kazi wa walimu.
Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Daladala cha Dar es Salaam (Darcoba), Sabri Mabruki alisema wamekubali kutoa usafiri bure kwa walimu ili kumuunga mkono Magufuli katika juhudi zake za kuboresha elimu. “Tumeletewa ombi na mkuu wa wilaya akitueleza kuhusu wazo la kutaka kusafirisha walimu bure. Kwa namna Makonda na Rais wanavyofanya kazi, hatukuwa na kinyongo zaidi ya kukubali ombi hilo,” alisema.
Akiunga mkono huduma hiyo, Mwenyekiti wa Umoja wa Wasafirishaji Abiria (Uwadar), William Masanja alisema elimu bure haiwezi kufanikiwa kama mazingira ya kazi ya walimu yatakuwa magumu.
“Ndiyo maana tulivyoambiwa na mkuu wetu wa wilaya, hatukuwa na muda wa kupoteza zaidi ya kukubali ombi lake. Tumejipanga kuwasafirisha walimu ili waweze kufundisha watoto wetu,” alisema.
Mwenyekiti wa Chama Wafanyakazi Madereva Tanzania (Tadwu), Shaaban Mdemu aliwataka walimu kuzingatia muda uliopangwa kusafiri bure ili kuondoa usumbufu.
Aliwataka wamiliki wa daladala kuwa wasikivu iwapo wataambiwa na madereva wao kuwa mapato ya siku yamepungua kutokana na kuwepo kwa huduma hiyo.
Akizungumzia uamuzi huo, Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiah Oluoch alisema jambo hilo likitekelezeka, Makonda atakuwa kiongozi wa mfano hapa nchini kuthamini kazi za walimu.
“Mpango huu unatakiwa kupongezwa, kuungwa mkono na wadau wa elimu. Tunahitaji kuwapa moyo viongozi wabunifu kama hawa,” alisema.
Alisema walimu wa Mkoa wa Dar es Salaam wanatumia wastani wa Sh3,000 kwa siku kwa ajili ya usafiri wa daladala.
 
“Sehemu kubwa ya mishahara ya walimu inatumiwa kwa ajili ya usafiri, mpango huu utakuwa mkombozi kwao,” alisema.
Alisema kama mpango huo utafanikiwa mkoani Dar es Salaam, unatakiwa kuanzishwa kote nchini.
Hata hivyo, Oluoch alipendekeza mpango huo utungiwe kanuni ili makubaliano hayo yaendelee kudumu hata kama viongozi hao hawatakuwapo Dar es Salaam.

MUUNGANO WA TANGANYIKA NA ZANZIBAR ULIVYOCHANGIA KATIKA UKUAJI WA KISWAHILI.
UTANGULIZI
Muungano ni hali ya kushikamana kwa vitu viwili au zaidi na kuwa kitu kimoja.(tuki 1981:288).
Kutokana na maana hiyo tunatambua kwamba Tanganyika ilikuwa ni nchi moja iliyojitegemea. Pia, Zanzibar vivyo hivyo. Tanganyika na Zanzibar zilikuwa nchi mbili tofauti kabla ya mwaka 1964, lakini 1964 ziliungana na kuwa nchi moja ni Jamhuri ya muungano ya Tanzania,inayojulikana kama Tanzania. (Sw.m. Wikipedia org 11/4/2015).
ASILI YA NENO KISWAHILI.
Neno Kiswahili lilianza kujitokeza katika maandishi ya zamani katika karne ya kumi na nne. Kwa mara ya kwanza lilijitokeza katika maandishi ya Ibn Batuta 1331KB. Neon hili lilitoka kwa waarabu waliokuwa wakifanya biashara na wenyeji wa pwani ya Afrika mashariki. Waarabu walianza kuupa upwa wa Afrika mashariki kalabu ya Kiswahili “sawahili” (sahel) kwa maana ya eneo la watu wa pwani na wenyeji wake wakaitwa “Sawahiliya” (Sawahel). Neno “sahel” baadaye lilibadilika na kuwa “Kiswahili”. (NASRI 0717029716) Masebo na Nyangwine 2002:67).
Kutokana na ufafanuzi huu tunaweza kusema kuwa Kiswahili si kiarabu bali ni lugha ya wabantu wa afrika mashariki mfano ushaidi wa kihistoria unathibitisha hilo (nchimbi 2008). Ingawa neno lenyewe Kiswahili lilitokea huko uarabuni.
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulichangia pakubwa katika ukuaji wa Kiswahili kama ifuatavyo:-
Kiswahili kilipewa hadhi ya kuwa lugha ya taifa hili la Tanzania1964. (Masebo na nyangwine 2002:67) (sw.m.wikipedia.org/wiki). Hali hii ilitokana na maono makubwa waliokuwa nayo waasisi wa taifa la Tanzania ambao ni Julius Kambarage Nyerere na sheikh Abeid Aman Karume. Waasisi hawa pamoja na watanzania waliokuwepo kipindi kile walipenda Kiswahili kukiheshimu. Hali hii ilikiwekea misingi mizuri ya lugha hii na leo inaendelea kukua kila kukicha. Hali hii imetokana na taifa la Tanzania kutumia lugha ya Kiswahili katika shughuli zao za kila siku.
Kiswahili kilipewa hadhi ya kuwa lugha rasmi nchini Tanzania.
Hadhi ambayo iliwezesha kutumika katika shughuli zote za kiserikali,kwa mfano shughuli za bunge, jeshi, mahakama na sekta mbalambali za kiserikali hususani kilimo. Matumizi haya yapo hadi sasa na yanazidi kushamiri katika nchi nzima.(sw.m.wikipedia.org).kufikia sasa Kiswahili ni utamaduni tosha wa taifa la Tanzania .Utamaduni huu unazidi kushamiri hadi nje ya taifa la tanzania na sasa, Kiswahili kinajulikana kama utamaduni wa afrika mashariki yaani Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi.kupitia Kiswahili tunaweza kutangaza muziki wa kitanzania ambao haupatikani katika taifa jingine ulimwenguni. Muziki huo ni taarabu, na mchirizi. Kupiti Kiswahili tumeweza kutambua binadamu wote ni sawa hakuna binadamu aliyemzidi mwenzie na kutegemeana kwa namna tofauatitofauti za kiuchumi,kisiasa,kijamii na kiutamaduni. Hivyo muungano unazuia ubaguzi, uchoyo na ukatili kupitia Kiswahili.
Waaidha Kiswahili kilipewa nafasi ya kuwa lugha ya kufundhishia katika shule za msingi, shule za upili na vyuoni nchini.
Katika shule za upili kinasomwa kama taaluma mojawapo. Aidha, Kiswahili kinatumika katika kufundishia vyuo vya ualimu ngazi ya cheti. Kiswahili kimepewa nafasi ya kufundishwa vyuo vikuu mfano hapa SAUT tunasoma Isimu ya lugha ya Kiswahili, fasihi ya Kiswahili na fasihi linganishi, ila bado Kiswahili hakijapewa kuna nafasi katika kufanyia utafiti.Pia, kuna vyuo duniani vinavyofundisha lugha ya Kiswahili vikiwemo vyuo vya Asia, mfano China kuna chuo kikuu cha mawasiliano na habari na vyuo vikuu vya lugha za kigeni vya Beiging na Tianjin, Marekani, kuna vyuo vya Yale, Harvard, chuo kikuu cha Indiana, chuo kikuu cha Georgia , Michigan state na chuo kikuu cha Illions.(Wa’njogu katika (www.gucosa-de/...15--10). Pia, uingereza nako kuna vyuo vinavyofundisha lugha ya Kiswahili (sluhwago.blogspot.com).
Kiswahili kimepewa nafasi na heshima kubwa kutumika katika vyombo vya habari.
Serikarili yao ilijitahidi kutoa fursa ya kuanzisha vyombo vya habari hasa radio mfano, radio Tanzania iliyoitwa redio Tanzania Dar-es- salaam (RTD) tarehe 1.7.1965 baada ya muungano. (www.tbc.go.tz 16.4.2015). vituo vya televisheni mfano , TBC, ITV, na Star TV. Magazeti mfano, gazeti la mtanzania, mwananchi na mwana spoti. Pia, Kiswahili kimevuka mipaka kinatumika katika kutolea matangazo na vyombo vya habari vya nje ya Tanzania na afrika ambavyo ni , BBC London, sauti ya ujerumani na sauti ya Amerika VOA.(sluhwago.blogspot.com) vyombo vya habari vilivyoanzishwa ni vya serikali na watu binafsi, lakini vyote hutumia lugha yya Kiswahili.
Licha ya yote Kiswahili kilipewa hadhi ya kutumika kuandikia katiba ya taifa letu la Tanzania 1977, katiba hii inapatikana katika www.bugando.ac.tz. Halikadharika, rasimu ya katiba pendekezwa pia imeandikwa kwa Kiswahili nayo inapatikana katika www.zanzibar.go.tz. Hivyo tunaona Kiswahili kilivyopewa hadhi kulik lugha zingine nchini Tanzania.
Vilevile Kiswahili kilipewa nafasi yya kutumika katika sherehe za kitaifa.
Sherehe hizi ni pamoja na sherehe zza muungano, jamhuri, kuwasha na kuzima mwenge wa uhuru ambazo hufanyika kila mwaka na huudhuriwa na wananchi wa Tanzania na wageni kutoka nje ya nchi. Wageni hawa hushawishika kujifunza Kiswahili angalau cha kuombea maji ya kunywa kutoa salamu.
Taifa la muungano la Tanzania linatambua michezo na huitunza kama sehemu ya utamaduni. Aina za michezo hii ni mpira wa miguu, mpira wa pete, riadha, masubwi, kuogelea, ngoma na muziki. Michezo hii huchangia kukua kwa Kiswahili kwa sababu wachezaji na waandalizi wa mchezo husika hutumia lugha ya Kiswahili kwa sababu wachezaji na waandalizi wa michezo husika hutumia lugha ya Kiswahili katika mawasiliano yao.
Katika kudumisha Kiswahili vyombo mbalimbali viliundwa ili kukuza na kueneza Kiswahili. Vyombo hivyo ni , taasisi ya uchunguzi wa kiswahili (TUKI) sasa inaitwa (TATAKI) mwaka 1964, chama cha usanifu wa Kiswahili na ushairi Tanzania (UKUTA) mwaka 1965, na baraza la Kiswahili la taifa (BAKITA) likiwa na jukumu la kukikuza na kukistawisha Kiswahili kama lugha ya Taifa.(jan,1999:93) n masebo 2002:67) pia mwaka 1981 ilitolewa kamusi ya Kiswahili sanifu toleo la kwanza n toleo la pili mwaka 2004. Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA) , pia, kuna baraza la kiswahili la afrika mshariki (BAKAMA).(sw.m.wikipedia.org/wiki/Kiswahili).
Nahitimisha kwa kusema hivi; kukua, kuendelea na kukomaa kwa Kiswahili, kumetokana na kuwepo kwa muungano wa Tanganyika na zanzibar. Pengine, kama muungano huu usingekuwepo, tusingefanikiwa katika matumizi ya lugha hii kwani kila upande ungeamua kutumia lugha za kigeni au za mkabila. Hivyo hatuna budi kulinda na kukienzi Kiswahili chetu.
MAREJEREO
TUKI (2004) Kamusi ya Kiswahili sanifu, (Toleo la pili).Dar es salaam:Oxford
University press.
Nchimbi A.S (2008), CHUO KIKUU HURIA CHA TANZANIA.DAR ES SALAAM:
Tasisi ya Elimu.
Masebo na Nyangwine (2002);NADHARIA YA LUGHA.Dar es salaam:Nyambari
Nyangwine Publishers.
Jan (1999) State Ideology and Language in Tanzania.



28 Feb 2016


KARIBU  MWANZA

Ndugu  zangu  mikoani, majirani  kadhaika
Marafiki  wa  shuleni,  na  nyumbani  bugarika,
Nipo  mwanza  mkoani,hapa hapa  bila  shaka,
Karibu  mwanza  karibu, mwenyewe  ujionee

Cha  kwanza  ni  wakarimu, wenyeji  nawasifia,
Kwa  utii  na  nidhamu,hiyo  sifa  yao  pia,
Mji  wa  mwanza  mtamu, una  vivutio  pia,
Karibu  mwanza  karibu, mwenyewe  ujionee


Mwanza  wenye  mji  wao,kwanza  nawapa  heshima,
Ahsante  kukaa  kwao, toka  nitoke  kwa  mama,
Niwataje  jina  lao, wengi  wao  wasukuma,
Karibu  mwanza  karibu, mwenyewe  ujionee

Hewa  safi  ya  ziwani, toka  kwenye  ziwa  lao,
Na  samaki  mchuzini, sato  kwao  kitoweo,
Karibu  kwao  nyumbani,  ujifunze  mambo  yao,
Karibu  mwanza  karibu, mwenyewe  ujionee

Leo  nakula  kasama, kuifafanua  mwanza,
Nyamagana  sengerema, karibu  nawaimiza,
Mje  kuona  milima, ile   wanayotangaza,
Karibu  mwanza  karibu, mwenyewe  ujionee

Kwa  wale  wenye  watoto, muwapeleke  mwanzao,
Watimize  zao  ndoto, kukutana  na  wanzao,
Wale  sangara  na  sato, wanenepe  miili  yao
Karibu  mwanza  karibu, mwenyewe  ujionee

Kuna  vitu  vingi  sana, karibu  ujionee,
Ilemela  nyamagana, na  misungwi  ujongee,
Cha  zaidi  mimi  sina , mwanza  mji  wa  pekee,
Karibu  mwanza  karibu, mwenyewe  ujionee.

27 Feb 2016




 NASAHA NA FASAHA ZA   
     SHAABAN ROBERT
KITABU: MAISHA YANGU NA BAADA YA MIAKA HAMSINI (UK 2)
 Shaaban Robert anasema:

 “………. Labda utashangaa mimi nilitaka sana bahati ya namna hii badala ya bahati ya vitu kama vile utajiri au mamlaka juu ya watu vinavyotafutwa na wengi kwa ajili ya fahari yake. Nasadiki utajiri ni kitu cha tamaa na mamlaka yanafahari lakini nilivihofu vitu hivi sababu pengine wenye vitu hivi kwa wingi na kufurika aibu iliwatia alama  mbaya sana.Niliona mamia ya watu walio uza roho zao kwa vitu hivi lakini pato lao lote lilikuwa ni uharibifu wa majina yao, Ukosefu wa jina zuri ni ukiwa mkubwa duniani jambo hili sikulipenda. Nilitaka niwe na jina lililo mbali na madoa katika umaskini na  unyonge wakati wote wa maisha yangu.
Jambo hili likiwa jepesi au gumu kumpa moyo mtu au uchovu, mimi nilikusudia kulipata kwa hali yeyote  kama nikishidwa kufaulu kupata lote nilitaka nipate nusu au robo yake. Kidogo bora kuliko kukosa kabisa; na jaribu dogo la wema bora kuliko kubwa la ubaya……….
                                                                                                                                              Bm mtillah 0717608 230
    


MKE  HAISHIWI  JAMBO

Ahsante mungu  mwenyezi, mambo  taka  niyaweke,
Niyaweke  waziwazi, heshima  ya  mwanamke,
Kwa vizazi  na  vizazi,waone  thamani  yake,
Mke  haishiwi  jambo, acha nafasi  anene.

Anene  jambo  kwa  wazi, hadharani  asikike,
Aeleze  yake  hadhi,  na ukweli  aanike,
Na  wenye  vipingamizi,zao  hoja  ziwatoke,
Mke  haishiwi  jambo, acha nafasi  anene.

Askari, mwanafunzi, lazima  aheshimike,
Ni  fundi  wa  kudarizi, na  vitabu  aandike,
Msimwekee  vitanzi, nambari  moja  ashike,
Mke  haishiwi  jambo, acha nafasi  anene.

Mtazame  kwenye  kazi, lazima  awajibike,
Anafaa  kila  ngazi, chini  juu  zote  zake,
Urubani, uuguzi, zote  taaluma  zake,
Mke  haishiwi  jambo, acha nafasi  anene.

Kwa  upande  wa  malezi,  hizo  nazo  sifa  zake,
Daima  ni  mtetezi , wa  ile  famili  yake,
Mke  jamani  mlezi, leo  wazi  niwaweke,
Mke  haishiwi  jambo, acha nafasi  anene.

Sasa  mke  vunja  zizi, huko  ndani  na  utoke,
Uwaseme  saaizi, mafasiki  uwachoke,
Watambue  zama  hizi, kutawala  mwanamke
Mke  haishiwi  jambo, acha nafasi  anene.

Na  suala  la  uongozi, ni  kubwa  nafasi  yake,
Kutunza   usimamizi, kuongoza  nchi  yake,
Haitaji  saidizi, bali  yeye  na  wenzake,
Mke  haishiwi  jambo, acha nafasi  anene.

Mila  potofu  za  enzi, zinohusu  mwanamke,
mziache  wanagenzi, mshike  nao  washike,
na  majukumu  ya  kazi, mpike  nao  wapike,
haki  sawa  itawale,  mke  kaongea  jambo.
Powered by Blogger.

Wasiliana nami papo kwa papo

Name

Email *

Message *

Ads 468x60px

Breaking News

Top Featured

Featured Posts

Sample text

Sample Text

Recomended

Facebook

Advertise

Most Popular

Connect With Us

Followers

Social Icons

Pages

Pages

BTricks

Pages

Popular posts

Tafuta chochote ukiwa hapahapa

Kategori

Recent Comments

You can replace this text by going to "Layout" and then "Page Elements" section. Edit " About "

recent posts

Video Of Day

TRANSLATE

Instructions

Video

Flickr Images

FURAHIA UWEPO WAKO HAPA

Logo Design by FlamingText.com
Logo Design by FlamingText.com

Imetembelewa mara

TAKWIMU ZA WATEMBELEAJI

Popular Posts

SAJIRI

Definition List

premium-wordpress-themes.org