30 May 2018








 
MAKALA FUPI YA DONDOO YA TAALUMA YA TAFSIRI NA UKALIMANI.
MAALUMU KWA WANAFUNZI WA KIDATO CHA 5 & 6.
SHULE YA UPILI AGAPE – MBAGALA.














IMETAYARISHWA NA :
MTILA BAHATI  NA   MPUNDA H. MUHIDINI
2018








Utangulizi
Kwanza, tunatanguliza shukrani zetu za dhati kwa Allah kwa kutujalia ilhamu, siha na raghba katika mchakato mzima wa kuandika Makala haya. Tusingefua dafu pasi na Baraka zake yeye.
Jitihada zetu za kuandaa Makala haya ya tafsiri na ukalimani ni za kweli, zilizojaa neema na nia ya kusaidia kusukuma gurudumu la elimu nchini Tanzania na katika jamii nzima ya Afrika Mashariki kwa ujumla.
Dondoo hizi chache katika Makala haya, zimehawilisha kutoka katika mswada mkuu wa kitabu cha masuala ya tafsiri na ukalimani kinachoandaliwa na waandishi Mtila bahati pamoja na Muhidini H. Mpunda. Kinachotarajiwa kuzinduliwa mwaka huu 2018. Pia dondoo hizi zimezingatia sana mahitaji ya wanafunzi wa shule ya upili AGAPE- MBAGALA baada ya kufanya mazungumzo na kuchangia mawazo kuhusu vipengele kadhaa vinavyochanganya katika taaluma hii ya tafsiri na ukalimani, hatimaye, kuamua kuyafanyia kazi mawazo yao ili kutatua changamoto hiyo.
Ni matumaini yetu dondoo hizi chache zinaweza kusaidia kwa namna moja au nyingine kutatua changamoto katika baadhi ya vipengele vichache tulivyovifanyia kazi.
Tutangulize shukrani zetu za dhati kwa mkuu wa shule kwa kutupatia ridhaa na kutukaribisha shuleni kwake, pili idara ya Kiswahili pamoja na walimu wengine wa shule ya sekondari Agape kwa ushirikiano wa hali na mali, baadhi yao ni mwl Bariki Kyando, Baraka Kalinga na Pendo Nicholous.
Mwisho, tunaitimisha kwa kusema Makala hii tunaitabaruku kwa walimu na wanafunzi wote wa kidato cha tano na sita kwa vizazi na vizazi watakaojiunga na shule ya upili Agape.

Mtila bahati
Barua pepe:bamtila@gmail.com
Blog: mtilabahati.blogspot.com
Rununu: 0675 975 756/0683 797 770
Dar- es- salaam

Mpunda H. Muhidini 
Barua pepe: muhidinimpunda@gmail.com
Rununu: 0656 984 873/0692 468 788
Dar- es- salaam




TAFSIRI
Maana ya Tafsiri
Tafsiri ni taaluma inayojihusisha na uhawilishaji wa mawazo au ujumbe ulio katika maandishi kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa kwa kusudi maalum.
Dhana za msingi katika tafsiri
Fasili ni kufafanua maana ya neno kwa kina.
Kurudufu ni kunakili alama au kitu kama kilivyo. Kwa hiyo, urudufu unaweza kuitwa ni unakili. Kwa mujibu wa TUKI (2013), kunakili ni kufuatisha au kutoa kivuli cha mchoro au maandishi kama yalivyo.
Ukafsiri ni mchakato wa kitendo cha kukafsiri. Kukafsiri ni kuhawilisha ujumbe kutoka matini andishi kwenda mazungumzo au kutoka mazungumzo kwenda katika maandishi kutoka lugha chasili hadi lugha lengwa, kwa kuzingatia muktadha, isimu na utamaduni wa lugha zinazohusika.Mfano mzuri ni sinema ambazo wahusika wake wanakuwa wanaongea lakini maneno yake yanaandikwa katika runinga chini.
Matini ni kifungu cha maneno kilichoandikwa ambacho kimebeba maana au ujumbe fulani.
Matini chanzi ni  matini inayotafsiriwa kwenda lugha nyingine
Matini lengwa ni matini iliyotafsiriwa katika lugha lengwa.
Lugha chanzi ni lugha iliyotumiwa katika mchakato wa kuandaa matini chanzi
Lugha lengwa ni lugha inayotumiwa katika mchakato wa kuunda matini lengwa.
Mfasiri mtu mwenye taaluma au tajiriba ya kutafsiri na ambaye amejikita katika shughuli hizo. Pia lazima awe mjuzi wa lugha zisizopungua mbili.
Nduni za mfasiri kabambe au jamali
Zifuatazo ni baadhi ya sifa au nduni za mfasiri jamali;
(i)                             Awe mwenye taaluma na ujuzi wa tafsiri mfano awe amesomea kozi ya taaluma ya tafsiri au amepitia mafunzo fulani,
(ii)                           Awe na utashi wa kuibua hisia sawa kwa wapokezi wa ujumbe.
(iii)                         Awe na tajiriba katika taaluma zingine mfano isimu jamii na isimu ethnolojia.
(iv)                         Awe mzawa au mbobevu wa tamaduni mbalimbali.Mwenye kipaji au taaluma ya uhariri, uandishi, na uhakiki wa matini mbalimbali.
(v)                            Awe na stadi za uhakiki matini.
(vi)                         Awe na maarifa au ujuzi wa teknolojia ya habari na mawasiliano yaani (TEHAMA)
(vii)                       Awe na tajiriba kubwa ya usomaji wa aina mbalimbali za tafsiri.
(viii)                     Awe na tabia yakushirikiana na watu wengine katika shughuli za kufasiri.


DHIMA ZA TAFSIRI
Tafsiri ina majukumu lukuki ndani ya jamii hususani katika ulimwengu wa sasa wa sayansi na technolojia. Baadhi ya dhima za tafsiri ni kama ifuatavyo :-
(i)                             Kueneza utamaduni wa jamii ya lugha chasili, kupitia kutafsiri kazi mbalimbali za kitaaluma pamoja na za kifasihi imesaidia kujua asili ya utamaduni wa lugha chasili. Mfano tamthilia ya “nitaoa nikipenda” imetungwa katika mazingira ya jamii ya kikuyu na kwa mara ya kwanza iliandikwa kwa lugha hiyohiyo lakini baada ya kutafsiriwa kwa kingereza (I will marry when I want) wasomaji wengi waliweza kujua mila na desturi za jamii ya wakikuyu.

(ii)                           Kutambua historia ya jamii husika, kazi nyingi sana za kale zilikuwa zimeandikwa katika lugha ya  eneo fulani mahususi. Mfano tamthilia ya Sofokile iitwayo
“ Mfalme edipode” iliandikwa kwa kigiriki kama lugha chasili ilifanikiwa kufanyanyiwa tafsiri kwa kiingereza na hatimaye katika lugha ya Kiswahili.

(iii)                         Tafsiri husaidia kujua itikadi ya jamii husika,
Itikadi ni imani kuhusu jambo fulani,waandishi wengi hupenda kuandika kazi  zao huku wakitanguliza itikadi mbele. Tafsiri inapochukua mkondo wake ndipo tunakuja kujua kumbe mwandishi fulani ana itikadi gani au jamii Fulani ina itikadi gani.

(iv)                         Tafsiri kama mbinu ya mawasiliano. Tafsii hutumika kutolea maelekezo ya biashara kama vile maelekezo ya jinsi ya kutumia bidhaa zinazouzwa na kusafirishwa kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine sanjali na matangazo ya kitalii. Pia, tafsiri hutumika katika vyombo vya habari  na katika vitabu vya kufundishia na kujifunzia.

(v)                           Tafsiri kama soko la ajira, wataalamu wengi wa tafsiri wanafanya kazi mbalimbali kama sehemu ya kipato na ofisi kwa ujumla watu hufanya tafsiri katika kazi mbalimbali mfano mikataba ya kimataifa, nyaraka za kiserikali ( sheria mbalimbali pamoja na katiba) na mashirika binafsi, pia tafsiri ya vitabu mbalimbali husaidia waandishi kupata kipato binafsi.


(vi)                         Tafsiri kama mbinu ya kujifunza lugha. Tafsiri hapa husaidia kukuza lugha lengwa mfano fasihi ya lugha lengwa hunufaika kwa kuingizwa kwa vipengele kadhaa vya lugha hususani misemo na methali ambazo hazikuwepo katika lugha hiyo lengwa.

(vii)                       Tafsiri hutumika katika nyanja ya elimu, sayansi na teknolojia, hapa tunaangalia maendeleo ya sayansi na technolojia ya nchi za Ulaya yametokana na maarifa yaliyoibiwa kutoka katika nchi za kiarabu mfano Misri. Watu wa Ulaya walifanikiwa kutafsiri vitabu na kujifunza maarifa na ujuzi wa watu wa Misri hatimaye nchi za Ulaya ziliendelea kupiga hatua. Pia nchini Tanzania mfumo wa elimumsingi unatumia lugha ya Kiswahili hivyo wataalam walilazimika kutafsiri vitabu kwa lugha ya Kiwahili ili viendane na lugha yao.

(viii)                     Kueneza na kuongeza wasomaji wa fasihi andishi, katika kila kona ya dunia kuna waandishi wa kazi za fasihi kutokana na watu wengi kutofahamu lugha nyingi husababisha watu kukosa maarifa mapya ya waandishi wengine, hivyo basi taaluma ya tafsiri imesaidia sana watu wa mataifa mbalimbali kusoma kazi moja ikiwa katika lugha mbalimbali mfano tamthilia, ya mfalme edipode imetafsiriwa katika Kiswahili kutoka Kiingereza wakati asili ya kazi hii ni Kigiriki.


(ix)                         Tafsiri kama kiliwazo cha nafsi ya mfasiri. Humfanya mfasiri kuutuliza mtima wake kadri anavyofanikiwa kutatua matatizo yake ya kifasiri. Utafutaji wa visawe katika lugha lengwa si kazi rahisi hivyo basi mfasiri anapopata visawe hivyo kutoka katika vyanzo mbalimbali  hufarijika kwa kupata mafanikio makubwa sana.

(x)                           Tafsiri imesaidia kuendeleza dini.Malenya (2016) dini ni imani ya mtu juu ya kitu fulani. Hapa tunaona maandiko mbalimbali yanayohusu masuala ya kidini yamefanyiwa tafsiri katika lugha mbalimbali mfano Biblia Takatifu iliandikwa katika lugha ya Kiebrania ikaambaa amba katika lugha mbalimbali mpaka kwenye kiingereza na hatimaye kwenye kiswahili na hadi kwenye lugha za makabila. Pia Qur- an Tukufu iliyoshushwa katika lugha ya kiarabu lakini mpaka hivi sasa kuna tafsiri nyingi katika lugha mbalimbali mfano Kiswahili na Kiingereza na Kijaluo. Mfano Profesa Omar Al Bashiri ametafsiri Qur- an tukufu kwenda Kijaluo
Mbinu au njia za Tafsiri
kielelezo kifuatacho kinafafanua njia zinazotumia kufanya tafsiri

                          MBINU ZA TAFSIRI

(i) Tafsiri ya neno kwa neno
Hii ni aina ya tafsiri ambayo mofimu (mofu) na maneno hufasiriwa yakiwa pweke pweke kwa kuzingatia maana zake za msingi bila kujali muktadha. Mdee, (1986:87) anasema, “Wafasiri aghalabu tafsiri zao huhitaji neno kwa neno katika dhana fulani badala ya maelezo.”   Katika aina hii ya tafsiri mpangilio wa mofimu na maneno ya lugha chanzi hubakia vilevile bila kubadilika..mifano,
Mfano 1.  Kiswahili: Alilala hadi asubuhi.
                 Kingereza: He/past/sleep/until/morning.
Mfano 2.  Kiswahili: Alikimbia mpaka ofisini kwake
                 Kingereza: He/past/run/until/office/his.
Mfano 3.   Kimakuwa:mustadi anolya ishima
                  Kingereza: mustadi/present/ eat/ugali.
Ubora wa mbinu hii
§  humsaidia mtu kuelewa muundo wa lugha chanzi na jinsi lugha chanzi inavyofanya kazi.
§  Husaidia kuelewa utofauti wa mpangilio wa maumbo katika sentensi za lugha tofauti.
Udhaifu wa mbinu hii
§  Upungufu  mkubwa wa njia hii ni kuwa, huwa haitoi maana lengwa kwa uwazi zaidi.
(ii)Tafsiri sisisi
Hii ni aina ya tafsiri ambayo maneno hufasiriwa yakiwa pweke pweke kwa kuzingatia maana za msingi katika lugha chanzi bila kujali sana muktadha lakini ni tafsiri inayofuata mfumo wa kisarufi hasa kipengele cha kisintaksia ya lugha lengwa. Ebu tuangalie mifano ifuatayo:
Kingereza: He was taken at the Central bus Station (bus)
Kiswahili: Alipelekwa kwenye kituo cha kati cha mabasi.
Badala ya kuwa: Alipelekwa stendi kuu ya mabasi.
Ubora wa mbinu hii
ü  Husaidia kufasiri dhana zisizofasirika kirahisi kama vile misemo, nahau, majina ya khanga n.k.
ü  Ni mbinu bora ukilinganisha na tafsiri ya neno kwa neno.
Udhaifu wa mbinu hii
ü  Si nzuri kutumika katika matini ndefu


(iii)Tafsiri ya kisemantiki                                                                             
Hii ni aina ya tafsiri ambayo mfasiri huegemea zaidi kwenye lugha chanzi. Katika aina hii ya tafsiri, mfasiri hufasiri kila neno katika sentensi jinsi lilivyo lakini kwa kufuata sarufi hususani vipengele vya kisemantiki na kisintaksia ya lugha chanzi. Inaitwa tafsiri ya kisemantiki kwa sababu, mfasiri anapofasiri hutakiwa kuweka mkazo kwenye maana ya matini kama ilivyokusudiwa na mwandishi wa matini chanzi.
Katika aina hii ya tafsiri, masahihisho au urekebishaji wa neno au jambo lolote unalodhani limekosewa hairuhusiwi isipokuwa unaweza kuweka hayo marekebisho au ufafanuzi katika tanbihi. Sasa tuanglialie baadhi ya mifano ya aina hii ya tafsiri:
Kiswahili: Alikwenda mpaka hospitali
Kingereza: He went up to hospitali

Kingereza: Aisha  married salumu
Kiswahili: Aisha alimwoa salumu

Faida ya mbinu hii
ü  Mbinu hii huingiza miundo ya misemo kutoka lugha chanzi. Mfano lugha ya Kiswahili imepokea miundo mipya ya misemo kutoka lugha ya Kingereza, baadhi ya miundo hiyo ni kama vile all ni all - yote kwa yote, at the end of the day – mwisho wa siku.
Udhaifu
ü  Tafsiri hii ni ya kimzunguko na ya kiufafanuzi sana.
ü  Haina vionjo na humfikirisha sana msomaji
(iv)Tafsiri ya mawasiliano
Ni aina ya tafsiri ambayo mfasiri ana uhuru wa kutumia visawe (maneno) yanayoweza kutoa athari sawa na ilivyo katika matini chasili. Kikubwa katika aina hii ya tafsiri hulenga kuhawilisha athari iliyopo katika matini chasili hadi katika matini lengwa.
Mfano,
Kiingereza: Tanzania National Electric Supply
Kiswahili: Shirika la Umeme Tanzania

Kiingereza: Wonders never end
Kiswahili: Ukistaajabu ya Musa utayaona ya Firauni.

Kiswahili : mwenda tezi na omo marejeo ngamani
Kiingereza: Go east, go west, home is best



Faharasa
Baadhi ya wataalamu wameelezea mbinu tano za tafsiri wakijumlisha tafsiri neno kwa neno, sisisi, semantiki (maana), mawasiliano na tafsiri mkopo
Tafsiri mkopo ni aina ya tafsiri amabyo mfasiri hutafsiri moja kwa moja mofimu za neno lililokopwa.





UKALIMANI
Maana ya Ukalimani
Ukalimani ni taaluma inayojihusisha na uhamishaji wa ujumbe fasaha ulio katika mazungumzo ya mdomo kutoka lugha chasili kwenda lugha lengwa.
Mkalimani ni mtu yoyote mwenye taaluma na tajiriba ya ukalimani na anayejihusisha na kukalimani.
Aina za ukalimani
Aina za ukalimani zinaweza kuanishwa katika vigezo vikuu viwili navyo ni:-
kigezo cha Muktadha au mazingira ya utendekaji wa tukio.
Kwa kujikita katika kigezo hiki cha muktadha na utendekaji wa tukio tunapata aina zifuatazo za ukalimani:-
Ukalimani wa Kijamii. Huu ni ukalimani ambao hufanywa katika masuala mbalimbali ya kijamii kama vile afya, ujenzi wa shule, maji, umeme na mihadhara ya kidini nk.
Ukalimani wa Mikutano na Makongamano; Huu ni ukalimani unaofanyika katika makongamano au mikutano mbalimbali. Mara nyingi aina hii ya ukalimani inafanyika katika mikutano ya kimataifa.
Ukalimani wa Mahakama.Aina hii hufanywa na wanasheria katika mahakama za ngazi mbalimbali. Pia huitwa ukalimani wa kisheria.
Ukalimani wa Kitabibu. Huu ni ukalimani ambao unafanyika mahali ambapo matibabu yanapatikana, kwa kiasi kikubwa aina hii ya ukalimani inafanyika katika hospitali kubwa.
Ukalimani wa Habari/katika vyombo vya habari; Huu ni ukalimani unaofanywa katika vyombo mbalimbali vya habari, hususani redio na televisheni ili kuiwezesha hadhira lengwa iweze nayo kuelewa matangazo yanayotolewa kwa lugha chanzi.
Ukalimani Sindikizi. Katika aina hii ya ukalimani, mkalimani hufuatana na mtu au kikundi cha watu katika safari au katika usaili au mahojiano. Mfano, wafadhili wanapoenda kuzindua miradi waliyofadhiri katika mataifa ambayo yanatumia  lugha ambayo ni tofauti na wanayozungumza, hususani vijijini lazima waambatane na mkalimani anayefahamu lugha ya wakazi wa pale pamoja na lugha ya mfadhili.
Kigezo cha Muundo au Mfumo wa Lugha.
Katika kigezo hiki tunapata aina  mbili za ukalimani. Katika kigezo hiki lugha inayotumika katika ukalimani inaweza ikawa lugha ya kusema/kuzungumza na lugha ya alama.
(i)                 Ukalimani andamizi      (ii) Ukalimani mtawilia

Ukalimani Mfululizo/Andamizi/sambamba. Ni aina ya ukalimani ambao mkalimani huzungumza takribani sambamba na mzungumzaji wa lugha chanzi.
Ukalimani huu ulifanyika kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Nurenberg, ambapo lugha kuu rasmi za kazi zilikuwa nne. Lugha hizo zilikuwa Kijerumani, Kiingereza, Kifaransa na Kirusi. Tangu wakati huo mahitaji ya ukalimani yamekuwa yakiongezeka kwa kiasi kikubwa.
Sifa za ukalimani andamizi.
ü  Katika ukalimani andamizi mkalimani anapeleka ujumbe kwenda lugha lengwa kwa haraka sana iwezekanavyo kama anavyouchukua kutoka lugha chanzi, huku mzungumzaji wa lugha chanzi akiendelea kuzungumza.
ü  Mkalimani huketi katika chumba maalum cha ukalimani (booth), ambacho hakipitishi sauti (sound proof).
ü  Mkalimani huzungumza kwa kutumia kipaza sauti huku akimwona na kumsikia mzungumzaji wa lugha chanzi kupitia visikizio.
ü  Hutumika katika makongamano ya kimataifa.
ü  Mashine ya kuhamishia ujumbe hutumika katika ukalimani andamizi.
ü   Aina hii ya ukalimani inahitaji usikivu na umakini wa hali ya juu.
ü  Mara nyingi wakalimani hubadilishana kila baada ya dakika 20 hadi 30 ili kupeana nafasi ya kupumzika.
ü  Aina hii ya ukalimani hutumiwa sana na vyombo vya habari mfano redio na runinga.

Faharasa
Ukalimani andamizi ni mbinu inayotumika katika ukalimani wa lugha ya alama. Hapo inapatikana aina nyingine ya ukalimani ambao ni ukalimani wa viziwi.

Udhaifu wa aina hii ya ukalimani.
ü  Njia hii ni hatari sana wakati mwingine mkalimani asiposikia vizuri anaweza kuacha maneno fulani ama kujitungia ili kufidia ujumbe uliompita.
ü  Mkalimani anakosa uhuru wa kukalimani atakavyo ili kuendana na kasi ya mnenaji chanzi.
Ukalimani mtawalia( Fuatishi). Hii ni aina ya ukalimani ambao mkalimani huzungumza punde tu mzungumzaji wa lugha chasili kumaliza ujumbe wake wakati mwingine hata kama hajamaliza ujumbe wake, baada ya mazungumzo ya lugha chanzi hutulia kwa sekunde chache ili kumpisha mkalimani kufasili ujumbe.
Vigezo vya ukalimani mtawalia
·         Mara nyingi mzungumzaji wa lugha chanzi na mkalimani huwa wamesimama au kuketi sehemu moja.
·         Hutumika sana katika masuala ya kijamii mfano masuala ya kidini, mahakamani, n.k.
·         Mkalimani hupata sekunde chache za kutafakari ujumbe.
·         Wakati mwingine hupeana kipaza sauti kwa zamu
·         Mkalimani anahitaji kutumia akili kuhamisha ujumbe bila kupotosha.
Stadi za msingi katika ukalimani
Zifuatazo ni stadi muhimu katika zoezi la ukalimani:-
        i.            Lugha na mawasiliano mfano kuongea, kusikiliza, kuandika na kusoma
      ii.            Stadi ya kunukuu
    iii.            Stadi ya kumbukumbu
    iv.            Stadi ya kuzungumza hadharani (umahiri wa kuongea vizuri mbele ya hadhara).
Dhima ya ukalimani.
*      Ukalimani ni daraja linalounganisha watu wanaotumia lugha tofauti. Mfano, watu wanaotumia Kiswahili huweza kuunganishwa na watu wanaozungumza Kifaransa kwa msaada wa mkalimani.

*      Soko la ajira, watu mbalimbali hufanya kazi ya ukalimani katika mataifa mbalimbali hivyo hujipatia kipato na kuboresha hali zao za kiuchumi.


*      Ukalimani hunufaisha katika kueneza dini ulimwenguni. Mfano watu hutoka katika mataifa mbalimbali kwa ajili ya kueneza neno la Mungu, hivyo basi wakalimani huchukua jukumu la kufikisha ujumbe kwa walengwa kwa kufasiri ujumbe wa maneno kwenda kwenye lugha zao.

*      Ukalimani hutumika katika matangazo ya kibiashara na masuala ya michezo. Lengo kuu ni kufikisha ujumbe kwa wasioelewa lugha chanzi. Mfano hivi sasa matangazo ya mpira hususani ligi kuu ya mpira wa miguu nchini Uingereza utakuta yanatangazwa katika lugha mbalimbali tofauti na ilivyokuwa zamani. Pia taarifa mbambali za matukio duniani yanayoripotiwa na vyombo vya habari vya mataifa ya Ulaya, matangazo hayo hukalimaniwa katika lugha mbalimbali hususani Lugha za kiafrika na kurushwa hewani ili mataifa yao wapate habari ile ile.


*      Ukalimani husaidia kufikisha ujumbe kwa watu wasiojua kusoma lugha tofauti. Hapa ndio tunaona tofauti kubwa kati ya tafsiri na ukalimani, ukalimani haubagui mtu yoyoye anapata ujumbe sharti awe na uwezo wa kusikia tu lakini tafsiri sharti ujue kusoma

Ufanano baina ya tafsiri na ukalimani
Tafsiri na ukalimani ni taaluma mbili tofauti zinazolandana na kutofautiana katika vipengele kadha wa kadha. Vifuatavyo ni vipengele vinavyolinganisha taaluma hizi mbili ya tafsiri na ukalimani.
Lugha. Taaluma zote mbili zinahusisha lugha katika kulikamilisha kusudio lake. Tafsiri hutumia lugha ya maandishi wakati ukalimani hutumia lugha ya mazungumzo. Lakini kwa ujumla taaluma zote zinatumia lugha.
Vijenzi. Ukalimani na tafsiri taaluma hizi zote hujengwa na vijenzi vyake ambavyo ni matini chanzi, matini lengwa, hadhira, lugha n.k.Vijenzi hivi ni lazima viwepo ndipo uhawilishaji uweze kufanyika.
Changamoto. Changamoto za tafsiri na ukalimani zote karibu zinafanana kwa mfano changamoto ya tofauti za kiisimu, tofauti za kimazingira, tofauti za kiitikadi na dini, tofauti za kitamaduni. n.k.
Dhima. Hiki ni kigezo kingine kinacholinganisha taaluma ya tafsiri na ukalimani. Majukumu ya tafsiri yanafanana kabisa na majukumu ya ukalimani, mfano wa baadhi ya kazi ya tafsiri na ukalimani ni kukuza lugha, kuendeleza na kueneza utamaduni, kuunganisha watu wa jamii tofauti.
Sifa. Kuna baadhi ya sifa za tafsiri na ukalimani zinashabihiana kiundani kabisa baadhi ya sifa zinazofanana ni; taaluma zote hutumia lugha mbili katika zoezi zima la uhawilishaji, mkalimani au mfasiri lazima ajue utamaduni wa lugha lengwa na chanzi vizuri, mfasiri na mkalimani hawatakiwi kuegemea upande wowote, pia lazima wote wawe wachapakazi na kujituma.
Nidhamu na Maadili. Kwa upande wa kipengele hiki tutajikita zaidi kwa mfasiri na mkalimani kwa sababu wote maadili yao huwa yanafanana sana, hii ni kwa sababu taaluma hizi zinauhusiano wa karibu sana. Baadhi ya maadili anayotakiwa kuwa nayo mkalimani au mfasiri ni ;-
ü   Lazima ajitume na kufanya kazi kwa bidii.
ü  Awe mwenye kujua majukumu yake na taratibu za kazi.
ü  Ushirikiano na mshikamano kwa wafasiri wenzake.
ü   Lazima awe mwaminifu kwa mteja wake na matini anayoitafsiri pia. Asiwe na upendeleo wa aina yoyote.
Gharama. Taaluma hizi zote zinaambatana na gharama lukuki mfano, ukalimani katika mikutano ya kimataifa, wakalimani mbalimbali hufasiri lugha mbalimbali ili kuwezesha mawasiliano.Pia tafsiri mara nyingi hutozwa gharama kwa kuhesabu kurasa au maneno yaliyotafsiriwa.

Utofauti baina ya tafsiri na ukalimani
Utofauti kati ya tafsiri na ukalimani pia unajidhihirisha katika vipengele vifuatavyo;-
Maana,kama ilivyo taaluma ya tafsiri hujishughulisha na upelekaji wa mawazo yaliyo katika maandishi kutoka lugha chasili kwenda lugha legwa. Ilhali, ukalimani ni zoezi la kuhamisha ujumbe ulio katika mazungumzo kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa.
Mfumo wa lugha. Lugha inayotumika katika tafsiri ni lugha ya maandishi, hivyo basi kazi inayofasiriwa sharti iwe katika maandishi lakini, katika ukalimani lugha inayotumika ni ya mazungumzo ya  mdomo, muda mwingine huambatana na ishara.
Aina za tafsiri na ukalimani, kwa upande wa tafsiri tuna aina nne kuu za tafsiri ambazo ni; tafsiri ya neno kwa neno, sisisi , maana na mawasiliano. Kwa upande wa ukalimani tuna vigezo viwili, kigezo cha kwanza ni mazingira ya zoezi linapofanyika, hapa tunapata ukalimani wa kitabibu, ukalimani wa makongamano, ukalimani sindikizi, ukalimani wa kitaaluma, ukalimani wa kijamii, ukalimani wa habari au vyombo vya habari n.k. Kigezo cha pili ni muundo na mfumo wa lugha hapa tunapata ukalimani andamizi na ukalimani mtawalia.
Wahusika, wahusika wakuu hapa ni mkalimani na mfasiri, katika taaluma ya tafsiri mhusika mkuu anayeshughulikia mchakato mzima ni mfasiri na katika ukalimani anayesimamia shughuli zote ni mkalimani mwenyewe.
Hadhira, kwa upande wa tafsiri hadhira lengwa hapa ni wale tu wanaojua kusoma na kuandika kwani ndio pekee watakaoweza kung’amua kile kilichoandikwa licha ya matini kuandikwa kwa lugha wanayoizungumza, ilhali hadhira kwa upande wa ukalimani si lazima wajue kusoma wala kuandika, kitu kikubwa kwao ni kusikia na msaada wa kuona matendo ya mkalimani ilimradi lugha inayotumika wanaifahamu.
Ukongwe, taaluma ya ukalimani ni kongwe sana na imedumu kwa muda mrefu lakini, taaluma ya tafsiri imeibuka tu baada ya kugundulika kwa maandishi.
Muda, mchakato wa tafsiri unachukua muda mwingi sana kutokana na hatua zake zinazopitiwa kama vile maandalizi, uhawilishaji, usawidi wa rasimu ya kwanza, udurusu wa rasimu ya kwanza, kusomwa rasimu ya pili na mtu mwingine na mwisho kabisa usawidi wa rasimu ya mwisho. Lakini ukalimani unaweza kufanyika ndani ya siku hata masaa. kwa upande mwingine mkalimani ana muda finyu sana katika kujiandaa lakini mfasiri ana kuwa na muda wa kutosha kujiandaa.


Maswali ya ziada
1. Kwa kutumia mifano fafanua dhana zifuatazo kama zinavyotumika katika tafsiri
        i.            Tafsiri
      ii.            Ukalimani
    iii.            Ukafsiri
    iv.            Fasili
      v.            Kurudufu
2. Linganisha na linganua taaluma ya tafsiri na ukalimani.
3. Mchakato wa tafsiri hauna mwenyewe bali una hatua zenyewe. Jadili.
4. Jadili vigezo ya mfasiri kabambe ili kupata tafsiri muluwa.
5. Kwa kutumia mchoro fafanua mbinu nne (4) za tafsiri.
6. Tafsiri na ukalimani hutofautiana kimaana lakini zinalingana kimajukumu.
7. Jadili uhusiano uliopo baina ya tafsiri, ukalimani na taaluma zingine.
8. Tafsiri ni zoezi la uhawilishaji wa ujumbe na si ufananishaji wa maneno. Jadili
9. Jadili dhima tano za tafsiri katika fasihi linganishi.
10. Tofautisha kati ya ukalimani andamizi na ukalimani mtawalia.
11. Jadili asili na chanzo cha ukalimani.
13. Maendeleo ya tafsiri yamepitia vipindi mbalimbali. Fafanua dai hili kwa mifano muafaka.
14. Jadili vizingiti vya tafsiri katika muktadha mbalimbali.
15. Fafanua sifa nne za msomaji wa pili wa rasimu ya pili ya tafsiri.
16.  (a) Nini maana ya ukalimani?
       (b) Fafanua vigezo vya mkalimani bora
17. Eleza shughuli tano zinazojitokeza katika hatua ya urudusu wa rasimu ya kwanza ili kuunda rasimu ya pili.
18. Kwa kutumia mifano jadili ukale wa taaluma ya tafsiri.
20. Kwa kutumia mifano ainisha matini kwa kigezo cha dhima kuu za lugha.
21. Kwa usaidizi wa mchoro fafanua aina nne za tafsiri.
22. Fafanua dhana zifuatazo kama zinavyotumika katika taaluma ya tafsiri.
     (a) matini pokezi
      (b) tafsiri pana
     (c) tafsiri finyu
     (d) jamii ulumbi
     (e) matini asili
23. Chanzo cha ukalimani ni jamiiulumbi. Jadili
24. Badili sentensi zifuatazo kwenda kwenye kiswahili
     i. You can not teach an old dog new tricks.
     ii. Like father like son.
   (iii)Clothes don’t make the man.
iii.        As you sow, so you shall reap.
iv.                All good things come to at a straw.
v.                  Action speak lauder than words.
vi.                A burnt child dreads fire.
vii.              A bird in the hand is worth two in the bush.
25. Mfasiri ni msaliti. Jadili
26. Thibitisha kauli hii “kwa nini wafasiri wengi wanakosa vigezo vya kuwa wafasiri bora”
27. Tofautisha kati ya ukalimani sambamba na ukalimani mtawalia. Hoja tano.
28. Kwa kutumia hoja tano (5) fafanua mbinu bainifu za mfasiri   bora katika kazi ya kufasiri matini mbalimbali.
29. Tafsiri ni mchakato, bainisha hatua muhimu za mchakato wa tafsiri.
30. Kwa mifano kuntu, fafanua kingo zinazomfanya mfasiri kukosa tafsiri toshelevu.
31. Mfasiri anapojaribu kupiga hatua katika kazi yake anakutana na miba zinazomchoma na kuathiri ufanisi na kusababisha kuibuka na tafsiri tenge. Jadili
32. Taaluma ya tafsri na ukalimani ni mapacha wanaofanana zaidi. jadili
33. Taaluma ya tafsri na ukalimani ni mapacha wasiofanana. Jadili
34. Kwa kutumia mifano fafanua mikururu ya taaluma ya tafsiri.
35. “Taaluma ya tafsri ni zoezi la uhawilishaji wa ujumbe kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa”.Fafanua mambo ya msingi yanayopatikana katika fasili hiyo.

KWA MSAADA ZAIDI WA MAKALA KAMILI YA TAFSIRI NA UKALIMANI PAMOJA NA MAKALA ZINGINE. USISITE KUWASILIANA NASI:
Mtila bahati
Barua pepe: bamtila@gmail.com
Blog: mtilabahati.blogspot.com
Rununu: 0675975756/0683797770
Dar- es- salaam

Mpunda H. Muhidini 
Barua pepe: muhidinimpunda@gmail.com
Rununu: 0656 984 873/0692 468 788
Dar- es- salaam

5 comments:

  1. Good notes , congratulations I learned something new. Thanks

    ReplyDelete
  2. Nisaifieni ubora na udjaifu wa ukalimani kimuundo na kimawasiliano

    ReplyDelete
  3. Nisaidie uhusiano baina ya tafsiri na ukalimani na taaluma zingine

    ReplyDelete
  4. Nisaidie sifa tank za mkalimani wa lugha ya alama

    ReplyDelete
  5. Nisaidie uhusiano wa tafsiri na matawi mengine ya isimu

    ReplyDelete

Powered by Blogger.

Wasiliana nami papo kwa papo

Name

Email *

Message *

Ads 468x60px

Breaking News

Top Featured

Featured Posts

Sample text

Sample Text

Recomended

Facebook

Advertise

Most Popular

Connect With Us

Followers

Social Icons

Pages

Pages

BTricks

Pages

Popular posts

Tafuta chochote ukiwa hapahapa

Kategori

Recent Comments

You can replace this text by going to "Layout" and then "Page Elements" section. Edit " About "

recent posts

Video Of Day

TRANSLATE

Instructions

Video

Flickr Images

FURAHIA UWEPO WAKO HAPA

Logo Design by FlamingText.com
Logo Design by FlamingText.com

Imetembelewa mara

TAKWIMU ZA WATEMBELEAJI

Popular Posts

SAJIRI

Definition List

premium-wordpress-themes.org