21 Sept 2019


KING SOLOMON SCHOOL.
MTIHANI WA KISWAHILI GRADE 3.
Soma habari ifuatayo kasha jibu maswali yake hapo chini
Hapo zamani za kale kulikuwepo na kijana mmoja akiahamika kwa jina la juma. Alikuwa na sifa ya upole na mcheshi sana. Juma alipenda sana kufanya shughuli ya kukusanya mayai polini na kuwinda . alibahatika kuwa na wadogo zake sita ambao ni  Chido, sombo, katuli, chihele, sihili na rwazi.
Maswali
Hapo zamani kulikuwepo kijana akifahamika kwa jina la _________
Kijana huyo alikuwa na sifa zipi __________ na ____________
Juma alipenda kufanya shughuli zipi ______________ na ___________
Juma alikuwa na wadogo zake wa ngapi? _______ wataje majina ya wadogo zake _______ ________ _______ _______ _______ ________
Andika maneno yafuatayo katika umoja wake
Umoja                                               wingi
________                                         vyura
________                                         vyoo
________                                         upungufu
________                                          kuta
________                                          vinu
Malizia methali hizi.
Asiyesikia la mkuu ________________________
Haba na haba ____________________________
Asiye na mwana __________________________
Kuishi kwingi ____________________________
Tenda wema ___________________
Bora nusu shari _________________

Panga sentensi zifuatazo kuanzia ya kwanza hadi ya mwisho 1 – 5
1.    Walifahamika kwa jina la chuda na mbozi (    )
2.    Waliishi kwa upendo na furaha sana kila walipokwenda kuwinda (   )
3.    Hapo zamani palikuwepo na wawindaji wawili (      )
4.    Huo ndio urafiki wa kweli unavyotakiwa (     )
5.    Waligawana sawa kila walichokuwa wamewinda (    )







UTANGULIZI
Mkondo wa kijamaa ni mkondo  wa utunzi  na uhakiki wa Kazi za kifasihi unamuona  binadamu  kama uti wa mgongo wa kuwepo kwa ulimwengu na maana ya ulimwengu huo.Mkondo huu unaibuka kutokana na mawazo ya watu waliokuwa na itikadi na sera za ujamaa  kama Karl Max,George Hegel,Maxim Gorky.
Mkondo huu  ulipokelewa  nchini  Tanzania kutokana na kuanzishwa kwa  Azimio la Arusha lililozaliwa mwaka 1967 kwa madhumuni ya kuwa muongozo wa ufafanuzi  na utekelezaji  wa  itikadi na sera  za Tanzania ambao wakati huo ilikuwa imeamua kufuata siasa ya kijamaa.Hali hii ya mabadiliko ya kisiasa  iliathiiri vikubwa muktadha  wa  fasihi ya Kiswahili,Ushairi  ukifuatiwa  sana na tamthilia zilikuwa tanzu  za mwanzo kusawil i mabadiliko haya huku zikionesha  hamu na matalajio makubwa  yaliojengeka katika mioyo ya wananchi.Riwaya ilichelewa kidogo kupokea mabadiliko hayo.
MAKUNDI YA MKONDO WA KIJAMAA
>Kundi  la kwanza  waliuona ujamaa katika jicho la namna  wahenga  wetu walivyoishi  pamoja na  jamii  yetu  ilejelee  kule nyuma.Kundi  hili  kazi zao kwa kusawili maisha yaliyopita .Watunzi wake walikuwa na doto ya maisha yaliyopita.
>Kundi la pili liliona ujamaa kwa jicho la matarajio kwamba kuna ujenzi  wa  jamii mpya itakayoishi  vyema  kuliko  hii ya sasa .kundi hili liliandika kazi zao kwa kusawili ndoto  za wakati ujao.Watunzi wake walikuwa  na (prognosia)hamu,shauku au maono ya wakati ujao.
Riwaya  zenye  muelekeo  wa  kinostalgia ;Riwaya ya kwanza ni ile ya ‘’Mtu ni Utu’’ mwaka 1971 iliyoandikwa na George Mhina  miaka minne  baada ya azimio kutangazwa.Namna  riwaya  hii ilivyo  sawili ujamaa ni ile ya kimaubiri na kavu.Ilielekea kuwa kijitabu cha kiada cha ujamaa kilichotaka watu wafuate  itikadi  hiyo kwa imani  zaidi kuliko kuelewa misingi na mantiki yake.Hamu ya ndoto ya maisha ya kijamaa ya  wahenga  iko bayana,lakini namna ya kuyapata  maisha hayo haijajulikana  wazi  sana.                                                                  
Riwaya nyingine ni njozi za usiku  ya mwaka 197, iliyoandikwa na W.Seme,ambayo nayo inashadidia  mfumo wa maisha  ya  wahenga  kwa  kusisitiza ushirikiano.Mfano wa riwaya ya kiprognasia ni   kama vile ndoto  ya ndaria iliyoandikwa mwaka 1975 na J.Mgomoi  ikitazamwa kwa shauku ya mabadiliko  ambayo yataletwa na vijiji  vya ujamaa,mpango wa kuishi  pamoja  uliobuniwa  kama  sera mojawapo  ya ujamaa  ya kuleta  maendeleo  kwa  jamii.
Riwaya ya shida 1975, iliyoandikwa na N.Balissidya,riwaya  hii haikuandikwa  kwa  lengo la kuhamasisha  maisha ya pamoja  na ushurikiano tu bali kuonyesha  pia maisha ya vijijini ni bora kuliko ya mjini ,huenda madhumuni  yalikua kupambana  na  kasumba ya watu hususani  vijana waliokimbia vijijini na  kwenda mjini  ambako walidhani  wangeendesha au kupata  maisha bora zaidi kinyume  na  hivyo kwani  baada  ya  kufika huko  walipambana na maisha magumu  ambayo  agharabu  yangewaingiza katika  matatizo makubwa  mfano katika Riwaya ya shida mwandishi  anatuonyesha  Matika na Chonya waliokimbilia  mjini  na  hatimaye  kujiingiza  katika  mambo  mabaya kama umalaya kwa matika na wizi kwa chonya na hatimaye kufungwa.
                                                                                                                                            MIHIMILI   YA MKONDO  WA  KIJAMAA  
Baada  ya  kuangalia maana  ya mkondo  wa kijamaa na kazi mbalimbali za riwaya zilizo sawiri vyema  mkondo huu,kunabaadhi  ya mihimiri ya mkondo huu ambayo ni kama ifuatayo:
Wahusika  wa kimaendeleo,hawa  ni  wahusika wenye nia na malengo  ya kufanya  mapinduzi  katika  hali ya maisha yao  na  jamii kwa ujumla.Ni  wahusika  wenye nia  ya kumiliki  njia kuu za kuzalisha mali katika jamii yao.Mfano wa wahusika hawa ni Denge,Mwajuma na Yasmini katika kitabu cha VUTA N’ KUVUTE(UK 68)”…Sikiliza  sista hawa wakoloni  na vijibwa vyao  ni watu wapumbavu kabisa ,kwao kila mtu ni komnisti ukidai haki yako wewe ni komnist……”
Kusawili  matukio ya kihistoria,wahusika hutekeleza matendo yao kitabaka.Hufanya  hivi  au  vile bila kufahamu.Muhimu ni kwamba  tabaka la wateswaji  hujipa mamlaka na nguvu za kiuchumi,Mfano katika riwaya ya Shida iliyoandikwa nae N.Balisidya.
Huzingatia  maisha ya makabwela,Makabwela  wamechorwa na waandishi mbalimbali  kuonesha  kwamba  hawana budi kupigania  maisha yao kwa hali na mali ili kuhakikisha  wanauangusha utawala  wa mabwanyenye.Kwakutumia  riwaya ya VUTA  N’ KUVUTE  ya SHAFI  ADAM  SHAFI  mwandishi  anatuonyesha  hili kwa kutumia  wahusika kama Denge na kundi lake  walivyokua msitari wa mbele  kuhakikisha  kuwa  wanakabiliana na wakoloni  na  vijibwa  vyao  ipasavyo,mfano  muhusika mmoja  anavyosema  “wakati  tunapambana na adui lazima kutumia mbinu  zote tunazoweza  kuzitumia .Pale inapoyumkinika  kutumia mbinu  za dhahiri  basi tuzitumie  kwa kadri  ya uwezo wetu .Pale ambapo hapana budi ila kutumia mbinu ya siri kwani  mapambano yetu ni yavuta n’ kuvute”(uk113)
Binadamu  huonyeshwa  kiuyaknifu,Wahusika ambao hutumiwa kama vipaza sauti  vya watunzi  hupuliziwa  uhai mathalani  ni wanadamu wa kawaida  wanaoishi katika ulimwengu  tunaowafahamu.Hueleza  hali  halisi ya maisha  anayoishi  binadamu  katika jamii.Husema  wazi  maovu  na  mema  yanayotendeka  katika  jamii  kama kipaza sauti cha kufikisha  ujumbe katika jamiii  bila kuogopa  wala  kupotosha  chochote,mfano Denge katika vuta n’kuvute.   
Huonyesha  matumaini  juu  ya kizazi  cha binadamu,inaelezwa  kuwa  mtu   atakua  mshindi  au  ni  mshindi  dhidi ya unyonyaji  wa  aina yoyote.Mfano katika kitabu  cha  SHIDA  mwandishi(Balisidya) anaonyesha dhana hii kwa kutumia  wahusika  wawili  ambao ni shida  au matika  na  chonya  au sefu ambao walikutana na matatizo mengi  baada ya kukimbilia  mjini  na kufikia hatua ya kukata tamaa,tumaini  jipya  lilitokea baada ya kuijiwa na ndugu zao waliokua kijijini na kuelezwa kuwa miundo mbinu  kadha wa kadha ikiwemo ya kilimo ilikua imeshawekwa na kama  watarudi nyumbani  wataenda shirikiana   na  na wanakijiji  wengine ili kuhakikisha maendeleo  yanapatikana.Hivyo haya ni matumaini wanayopatiwa  vijana  hawa  baada ya kukumbwa  na maswahibu mengi  na ndo moja kati ya mihimili ya  mkondo wa kijamaa.
Lugha inayotumiwa huendeleza malengo na mapendekezo ya walio wengi, katika mkondo huu msaniii  hutumia  lugha rahisi  na inayoeleweka  kwa kila tabaka  la wanajamii.Lugha inayotumiwa hupaza  sauti  ya kueleza matakwa  ya waliokuwa wengi  ambapo lengo kuu huwa ni kuleta usawa.
Muundo rahisi,Muundo wa riwaya katika mkondo huu  mara nyingi huwa ni wa moja kwa moja  wenye msuko wa matukio  ulio rahisi , wahusika  wasio  tata  wengi wao wakiwa  bapa.Wengi  wa hadhira yake  ni wanafunzi wa  shule za upili.
Hitimisho,mkondo  huu  unabani  na kujaribu kuonyesha  faida  ambayo inaweza patikana endapo watu wataishi kwa kushirikiana.Kupitia kazi za waandishi  mbalimbali  tunaona namna wanvyopambana  na jamii  zenye matabaka na unyonyaji  ambao kwa namna moja ama nyingine si haki na si chanzo cha maendeleo kwa jamii yote kwa ujumla.Mkondo huu  vile vile unajaribu kusimamia msimamo wa kuishi kama walivyoishi  watu  wa zamani kwani  walishirikiana  katika uzalishaji na kile kilichopatikana kilitumiwa na watu wote kwa pamoja.Hivyo basi mkondo huu unapigania usawa katika jamii  kwa ujumla.





MAREJEREO
Madumulla J.S,Riwaya ya Kiswahili,Nadharia,Historian a misingi ya uchambuzi;Dar es salaam:Mtule Education Publishers.
Njogu.K na Wafule,R.M(2007)Nadharia za uhakiki  wa fasihi :Nairobi:The Jomo  Kenyatta  Foundation.
Malenya.M.M(2008)Matumizi  ya  lugha  na jazanda,Nyimbo za  marehemu  Jacob Luseno.Tasnifu ya uzamili.Nairobi:Chuo kikuu cha Kenyatta. 























SWALI:  
Neno na sentensi ni vipashio vikuu katika sarufi mapokeo. Eleza kinaganaga aina ya maneno na sentensi kwa mujibu wa sarufi hiyo.


Sarufi mapokeo
Kwa mujibu wa Khamisi na Kiango (2002), sarufi mapokeo ni sarufi ya kale, wataalamu wanaohusishwa na mkabala huu walijitokeza kuanzia karne ya 5 Kabla ya Kristo na katka karne ya 18 na 19 Baada ya Kristo, wataalamu hao ni kama Plato, Aristotle, Panin na Protagoras ambao walijihusisha na lugha kwa kutaka kujua asili yake ikiwa ni sehemu ya uchunguzi wa asili ya maumbo, hususani walitaka kujua asili yake ikiwa ni sehemu ya uchunguzi wa asili ya maumbo, hususani walitaka kujua kama lugha ni tukio la kimaumbile au tukio la unasibu.
Massamba na wenzake (2009) wanaeleza kwamba sarufi mapokeo zilikuwa ni sarufi elekezi ambazo zilisisitiza kanuni na nini cha kusema na wajua lugha. Watu wasiojua kanuni za lugha wanapaswa kujifunza kutoka kwa wanaojua sarufi ya lugha. Wanaendelea kusema kuwa wanaojua lugha hupaswa kutunga kanuni za sarufi.
Waasisi wa sarufi mapokeo walikuwa ni wanafalsafa wa Ugiriki. Katika kipindi hiki sarufiilshughulikiwa sambamba na falsafa, dini, fasihi, balagha na mantiki. Waasisi hao ni Plato na mwanfunzi wake Aristotle (Matinde, (2012).
Kwa mujibu wa sarufi mapokeo ni kweli kwamba neno na sentensi ndivyo vipashio vikuu katika sarufi mapokeo. Vipashio hivi (neno na sentensi) vimefafanuliwa kwa undani na wanasarufi mapokeo kama tutakavyoona hapa chini.
Aina ya sentensi kwa mujibu wa sarufi mapokeo
Sentensi ni fungu la maneno lenye uarifishaji mkamilifu. Sentensi huwa na muundo uliokamilika na hujitegemea kimaana (Matinde, 2012). Pia Massamba na wenzake (2009:136), wanasema sentensi ni kipashio kikubwa kabisa cha kimiundo chenye maana kamili. Miundo ya sentensi huhusisha vipashio vingine vidogo kimiundo.
Kwa mujibu wa Matinde (2012:211), tunaarifiwa kwamba Plato aligawa sentensi katika sehemu kuu mbili: Mtenda (Subject) na Kitendwa (Object). Pia Massamba na Wenzake (2009:52) katika SAMIKISA wanaongeza kwamba uchambuzi huo ulizingatia zaidi uamilifu (kazi) wa faridi au vipashio mbali mbali katika tungo au sentensi.
Kwa mfano, sentensi “Mama anapika chakula” aliigawa sentensi hii kama ifuatavyo:
Mama
anapika chakula
Mtenda (Subject)
Kitendwa (Object)

Kwa mujibu wa Habwe na Karanja (2004:142) wanasema wanasarufi mapokeo waliainisha sentensi kwa mujibu wa uamilifu wake. Na baadhi ya makundi ya uainishaji yaliyojitokeza ni kama yafuatayo:
Sentensi taarifa (arifu)
Matinde (2012:160), anafafanua kuwa “sentensi arifu ni sentensi ambazo hutoa taarifa au ujumbe fulani.” Sentensi za aina hii huishia kwa kituo kikuu/nukta. Mifano ya sentensi arifu:
v  Baba amenunua kitabu.
v  John anaimba vizuri.
Sentensi agizi (amrishi): Hizi ni sentensi ambazo huamrisha au humwagiza msikilizaji kutenda kitendo/jambo fulani. Sentensi hizi huundwa na kitenzi cha kuamuru. Aghalabu sentensi hizi huwa na sehemu ya kitendwa (kiarifu) tu. Sentensi hizi huishia na kituo kikuu au mshangao (Matinde, 2012:160). Kwa mfano:
v  Leta hiyo sahani.
v  Nenda kapige kelele huko nje.
Sentensi ulizi (swalifu): Sentensi hizi huwa zina pengo katika sehemu yake ya taarifa. Hivyo hutaka kupata taarifa Fulani. Hizi ni sentensi ambazo uamilifu wake ni kuuliza swali. Sentensi swalifu huishia kwa alama ya kuuliza (?). Kwa mfano:
v  Mwanao ana umri gani kwa sasa?
v  Ndama amepotea lini?

Matinde (2012:161) ameongeza aina za sentensi zifuatazo kwa kuzingatia kigezo cha uamilifu wake ambazo ni hizi zifuatazo:
Sentensi mshangao
Matinde (2012:161) anasema sentensi mshangao ni sentensi ambazo hudhihirisha mshangao wa msemaji kuhusu jambo au hali fulani. Sentensi hizi huishia kwa alama ya mshangao. Mifano:
v  Juma amefeli!
v  Chakula kimeshapikwa!
Sentensi shurutia
Kwa mujibu wa Matinde (2012:161) anaeleza kuwa sentensi shurutia ni sentensi za masharti ambazo huundwa na vitenzi viwili. Kitenzi cha kwanza hukamilishwa na kitenzi cha pili ili kuonesha uhusiano wa masharti. Vitenzi hivi huambikwa viambishi vya masharti mathalani: -nge, -ngali, -ngeli, na -ki. Viambishi hivi ni nguzo ya sentensi shurutia. Kwa mfano:
v  Juma angelisoma kwa bidii angelifaulu mtihani
v  Jane angaliimba angalipata zawadi
Aina za maneno kwa mujibu wa sarufi mapokeo
Baada ya kuwa tumeona namna sarufi mapokeo ilivyoshughulikia suala la sentensi kwa kuigawa katika sehemu kuu mbili yaani kiima (Mtenda) na kiarifu (Kitendwa) na sasa tuone namna wanasarufi mapokeo walivyojishughulisha na maneno na aina zake kama kipashio kingine cha msingi kwa mujibu wa kigezo hiki. Massamba na wenzake (2009:54) wanasema aina za maneno zilikuwa ni nomino, Kitendo (Kitenzi), sifa (kivumishi), advebo (kielezi) n.k. (maneno yaliyowekwa kwenye mabano ni istilahi za siku hizi).
Kwa mujibu wa Matinde (2012:211-212) anaeleza kuwa mara baada ya Plato kugawa sentensi kugawa sentensi katika sehemu kuu mbili mtenda (Subject) na kitendwa (Object), Aristotle aliweza kwenda mbali zaidi ya kazi ya mwalimu wake Plato kwa kugawa sentensi katika sehemu kuu tano, ambazo ni; Nomino, Kitenzi, Kivumishi, Kiunganishi, na Kielezi.
Matinde (2012:212) anaendelea kueleza kuwa miaka 100 Kabla ya Kristo mwanasarufi Myunani Dionysus Thrax aliandika kitabu cha sarufi cha awali kabisa ambacho kiliitwa Techne Grammatike (The art of Grammar). Dionysus Thrax aliainisha sehemu saba za sentensi ambazo ni; Nomino, Kitenzi, Kivumishi, Kiwakilishi, Kiunganishi, kielezi, na  Kiingizi.
Pia Habwe na Karanja (2004:131) wanasema wanasarufi mapokeo waliainisha maneno kutokana na kazi ambazo maneno hufanya katika uundaji wa sentensi. Maneno haya yameainishwa katika makundi tofauti kulingana na maana na utendaji kazi wake. Uainishji wa awali wa aina hii ulifanywa na wanasarufi mapokeo ambao walitambua aina mabalimbali za maneno walizoziita kategoria za maneno.
Baadhi ya kategoria walizotambua ni: Nomino, Vitenzi, Viwakilishi, Vivumishi, Vielezi, Vihusishi, Viunganishi, Vihisishi, Vionyeshi, Vibainishi na kadhalika.   
Nomino: Kwa mujibu wa sarufi mapokeo ni neno la kutaja vitu- yaani ni majina ya vitu. Hivyo majina nomino hutaja majina ya vitu, watu, hali, mahali, vyeo, na dhana. Baadhi ya wanasarufi huita nomino majina. Mifano ya nomino ni kama vile Tanzania, Utundu, Mtoto, Kisu, Malaika na nyinginezo.
Mfano: Baba analima
Viwakilishi: Ni maneno ambalo hutumiwa kusimama badala ya nomino katika sentensi. Viwakilishi pia hujulikana kwa jina la pronomino. Mifano ya viwakilishi; Wapi unaenda?  Neno wapi ni kiwakilishi kiulizi, aina nyingine ya viwakilishi ni viwakilishi nafsi, viwakilishi vimilikishi, viwakilishi vya idadi, viwakilishi vya jumla na kadhalika.
Vivumishi: Vivumishi hueleza habari ya kitu au mtu kikionyesha jinsi mtu au kitu kilivyo. Kisintaksia kivumishi ni neno linalotoa sifa ya neno au kifungu cha maneno, aghalabu nomino na viwakilishi vyake.
Mifano;  Mzee mrefu amewahi.
               Kitabu kizuri kimepotea.
Vitenzi: Ni maneno ambayo huwakilisha kitendo.Mbaadu (1985) anaeleza kuwa vitenzi kama maneno yoyote yanayoonyesha mambo yanayofanywa na watu, wanyama, au vitu katika wakati fulani. Pia vitenzi hueleza hali Fulani za watu, vitu, na matukio. Vitenzi ni kama vile imba, cheza, lima, sema, soma na kadhalika.
Mfano; Mama analima shamba.
              Watoto wanaimba nyimbo zao vizuri.
Vielezi: Ni maneno au fungu la maneno ambalo huongeza maana ya kitendo. Ni maneno yanayofafanua vitenzi, vivumishi, na vielezi vingine.  Mifano ya vielezi ni kama vile sasa hivi, ovyo ovyo, asubuhi na mapema.
Mfano; Mwanafunzi ameondoka sasa hivi.
             Jack anacheza vizuri.
Vihusishi: Ni neno aukundi la maneno yanayohusisha sehemu mbili au zaidi za sentensi. Huonesha uhusiano baina ya kitu na kingine au mtu na mwingine kama wahusika katika sentensi. Mifano ya vihusishi ni maneno kama vile katika, juu ya, kwa, hadi na kadhalika.
Mfano; Omari anacheza juu ya kitanda.
              Mtoto anakula kwa kijiko.
Viunganishi
Ni maneno ambayo huunganisha maneno au mafungu ya maneno. Viunganishi huweza kuunganisha maneno na maneno, au maneno na vikundi vya maneno na vikundi vingine vya maneno. Mifano ya maneno ambayo ni viunganishi ni kama vile na, kisha, na kadhalika.
Mfano; Juma na Ali wanasoma. (Neno kwa neno). 
             Ali alikwenda maktaba kisha akasoma jarida. (kishazi na kishazi)

Vionyeshi
Kwa mujibu wa Kapinga (1983) vionyeshi ni maneno yanayoonyesha ujirani wa kitu kwa kukihusisha na kitu kingine. Vionyeshi pia vimerejelewa kama viashiria. Mifano ya vionyeshi ni kama huyu, wale, hao na vinginevyo.
Mfano; Wale wanakuja.
              Hao ni wazuri.
Vihisishi: Ni aina ya maneno ambayo huonyesha hisia kama vile hali ya kufurahi, uchungu, kushangaa, kushtuka na kadhalika. Awali vilijulikana kama vishangao lakini hii haikutosheleza jukumu la vihisishi kwa sababu vishangao ni aina moja tu ya vihisishi yaani vile vinavyoonyesha mshangao tu. Mifano ya vihisishi ni kama alhamdulillahi!, Mungu wangu! Ebo! Simile! Lahaula! na vinginevyo.
Mfano wa kihisishi; Mungu wangu! Amepotea?
Vibainishi: Kategoria hii haipokatika lugha ya Kiswahili. Huweza kupatikana katika baadhi ya lugha ikiwemo lugha ya kiingereza. Vibainishi hutumiwa pamoja na nomino.
Kwa mfano: The student ate all the food,   An elephant is a wild animal.
                   A book is a good thing to have.
Hivyo ndivyo ambavyo wanasarufi mapokeo walivyoweza kuainisha maneno na sentensi ambavyo ndivyo vipashio vya msingi vya lugha kwa kuzingatia kigezo hiki cha sarufi mapokeo. Kikubwa ni kwamba wao katika uainishaji wao waliegemea zaidi uamilifu wa tungo hizo yaani kazi ambazo maneno na sentensi hufanya.




MAREJELEO
Habwe, J. & Karanja, P. (2004). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers Ltd
Khamis, A. M. & Kiango, J. G. (2002). Uchambuzi wa Sarufi ya Kiswahili. Dar es salaam:
                  TUKI.
 Massamba, D. P. B. na wenzake (2009). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu (SAMIKISA):
                   Sekondari na Vyuo. Dar es salaam: TUKI.
Matinde , R. S. (2012). Dafina ya lugha isimu na nadharia: Kwa Sekondari, Vyuo vya Kati na
                   Vyuo Vikuu. Mwanza: Serengeti educational publishers


SWALI
1. Dadavua maana ya dhana mawasiliano kwa kurejelea nadharia mbalimbali.
2. Istilahi stadi za mawasiliano hufafanuliwa kwa kuzingatia nadharia mbalimbali.  
    Jadili

1. Dadavua maana ya dhana mawasiliano kwa kurejelea nadharia mbalimbali.
Kwa mujibu wa Kavoi na Wanjala (2013) wametafasili dhana  mawasiliano ni kitendo cha uwasilishaji  na ung’amuaji  wa maana kati ya watu au jamii kwa kutumia mfumo  wa ishara na miondoko iliyokubalika  katika  jamii mahusisi.
Dhana  mawasiliano imejaribu kuelezwa katika  kitabu cha “stadi za mawasiliano” katika nadharia kuu tatu kwa namna tofautitofauti kwa mujibu wa vijenzi pamoja  na uchangaano wake.Nadharia  hizo zinazojaribu kuelezea maana ya dhana mawasiliano finyu,mawasiliano mauluti na mawasiliano mihamala.
Nadharia  ya mawasiliano fingu; iliyoasisiwa na  Shampon,C.E na Weaver,W(1949).walitafasili mawasiliano  kwa upande mmoja tu yaani mawasiliano na simu.Aina hii ya mawasiliano fingu inahusu vipengele vitatu ambavyo ni mtoa ujumbe,ujumbe na mlengwa.Nadharia hii hutuumiza zaidi katika  shghuli za utawala.waasisi  hawa pia walibainisha  kuwa kelele  ndio chanzo kikubwa  kinachokwamisha mawasiliano.vilevile nadharia hii imeshindwa kuonyesha marejeo ya ujumbe anaotumia  mtoa ujumbe kwenda  kwa mlengwa.
Pia waitifaki wameweza kuelezea dhana ya mawasiliano kwa kutumia nadharia ya mawasiliano mahuluti waitifaki wameichukulia aina hii ya mawasiliano kuwa kwa kiasi fulani ni kamilifu,mawasiliano mahuluti huhusisha vipengele vitano ambavyo ni mtoa ujumbe,ujumbe,nyenzo,mpokea ujumbe na jibu.Aina hii ya mawasiliano huonyesha namna mtoa ujumbe  anavyogusana  na kuingilia  na mpokea ujumbe kupitia majibu yanavyotolewa,ili kuwa na mawasiliano timilifu katika uhusiano wa mtagusano mtoa ujumbe na mpokeaji  ujumbe  hubadilishana  nafasi.Nadharia hii ni mari zaidi ila hainyooshi uhalisia wa uchangamani  wa mchakato  wa mawasiliano.
Waitifaki wa nadharia hii ya mawasiliano mhamala wanadai kuwa wahusika katika mchakato wa mawasiliano huwa hawapeani zamu ya kutoa ujumbe,kuupokea ujumbe wala kutoa jibu.Waasisi hawa wanaamini  kuwa hutokea kwa wakati mmoja wao huchukulia mawasiliano kama mfumo wenye hatua madhubuti na unaojengwa  kwa mihimili inayotegemea,mihimili hiyo ni ujumbe,nyenzo,mtoa ujumbe,mlingwa,jibu,muktadha wa mawasiliano, idadi ya wahusika tajriba(utamaduni) ya wahusika na hali ya upokeaji na wawasilishaji.
Kwa ujumla mchakato wa mawasiliano unahusisha hatua saba ambazo zimefumwa katika shuka  la muktadha na wahusika .ujumbe,nyenzo,mtoa ujumbe,usimbaji,mpokeaji ujumbe,usimbuaji na jibu kwa hiyo stadi za mawasiliano zinahitajika  muda wote wa mchakato wa mawasiliano.



2. Istilahi stadi za mawasiliano hufafanuliwa kwa kuzingatia nadharia mbalimbali. Jadili
Istilahi” Stadi za mawasiliano” imetokana  na tafsiri  ya istilahi “Communicaion skills” ya kiingereza ,Baaadhi ya watu wameitafasili kama “Mbinu  za mawasiliano”Kimakosa.Istihali za “Stadi za mawasiliano” imeweza kufafanuliwa  au kutafasiliwa katika  nadharia  tatu kuu zinazojaribu kuitafasisi istilahi hii ambozo ni nadharia ya umilisi, nadharia ya ujaminishaji na nadharia ya utawala taarifa na mawasiliano.
Katika kitabu cha Stadi za mawasiliano waitifaki walioweza kuielezea  nadharia ya umilisi,  ni pamoja na Smith,Caput,Cupach,Spitznerg,Crettenden na Rawstone wao wanashikilia  kuwa Stadi za mawasiliano humwezesha mwasilianaji kuchajua mbinu stahili ya mawasiliano ili aitumie kuwasilisha  ujumbe  kwa mujibu wa muktadha husika.Nadharia hii inashikilia kuwa mwasilianaji anayemudu Stadi za mawasiliano  anafaa kuwa na hekima,maarifa na motisha inayomwezesha kuteua  nyenzo  tatu za kubeba ujumbe katika muktadha unaofaa,Pia nadharia hii imejengwa katika nguzo kuu nne ambazo ni hekima,motisha,maarifa na muktadha ambozo mwasilianaji anapaswa kuzizingatia  ili aweze kufikisha ujumbe ilivyokusudiwa
Nadharia ya ujiaminishaji; nadharia hii iliasisiwa na  William Gudykunst mwaka 1985,Waitifaki  wake wanadai kuwa maingiliano ya wawasilianaji  wakiwa katika  mchakato wa mawasiliano  hugubikwa na hali ya wasiwasi,uoga na mashaka hususani katika hatua za mwanzo.Hali hii hutokea  zaidi iwapo  wahusika hawafahamiani au wanatofautiana kihadhi,kiumri na kielimu au kikabila,Nadharia  hii hudai kuwa mwasilianaji ambaye anamudu Stadi za mawasiliano anapaswa kuwa na uwezo wa kudhibiti na kushinda hali ya mashaka udhibiti huo huwajengea  wawasilianaji hali ya kujiamini.
Nadharia ya utawalaji taarifa na mawasiliano; waasisi  wa nadharia hii ni pamoja  na De Ridder,Ballinger na De sai. Waitifaki wa nadharia hii wanashiliki kuwa  Stadi za mawasiliano huwawezesha wawasilianaji kubadilishana,kushilikishana na kutumia ujumbe husika pamoja na kuzalisha taarifa mpiga kwa hiari katika mchakato wa mawasiliano.
Kwa ujumla majumuisho ya nadharia hizi yanapatikana katika maoni ya mwanaisimu Cooper (1980) anyesema kuwa mtu anayezimudu  Stadi za mawasiliano ni Yule anayeweza kusema kile anachotaka kukisema na kumaanisha  kile  anachosema bila kupoteza  maana au kuleta utata wowote ule.
MAREJELEO
Wanjala, F.S na Kavoi, J. M. (2013). Stadi za Mawasiliano na Mbinu za Kufundishia  Kiswahili.
               Mwanza: Serengeti Educational Publishers  Ltd
Kiura, M. K. & Munga, E. C. (2010). Communication Skills. Mwanza: Serengeti Educational
                  Publishers Ltd.

   


Powered by Blogger.

Wasiliana nami papo kwa papo

Name

Email *

Message *

Ads 468x60px

Breaking News

Top Featured

Featured Posts

Sample text

Sample Text

Recomended

Facebook

Advertise

Most Popular

Connect With Us

Followers

Social Icons

Pages

Pages

BTricks

Pages

Popular posts

Tafuta chochote ukiwa hapahapa

Kategori

Recent Comments

You can replace this text by going to "Layout" and then "Page Elements" section. Edit " About "

recent posts

Video Of Day

TRANSLATE

Instructions

Video

Flickr Images

FURAHIA UWEPO WAKO HAPA

Logo Design by FlamingText.com
Logo Design by FlamingText.com

Imetembelewa mara

TAKWIMU ZA WATEMBELEAJI

Popular Posts

SAJIRI

Definition List

premium-wordpress-themes.org