14 Jul 2025

 

Lugha na Utamaduni

Dhana ya Lugha

Binadamu huwasiliana kwa kutumia lugha. Lugha ndicho chombo kikuu cha mawasiliano ya binadamu. Lugha ni miongoni mwa vitambulisho vya utamaduni wa jamii fulani. Jamii hutumia lugha kusalimiana, kupashana habari na kubadilisha mawazo. Ushirikiano baina ya mtu na mtu hutokana na matumizi ya lugha 

Kwa ujumla tunaweza kufasili lugha kwa kusema Lugha ni mfumo wa sauti za nasibu za kusemwa zenye maana zilizokubaliwa na jamii ya watu ili ziweze kutumika katika mawasiliano yao.

        Ni muhimu kutambua kuwa lugha ni kwa ajili ya binadamu na wala si kwa wanyama. Wanyama, wadudu na ndege huweza kuwasiliana miongoni mwao lakini hawana lugha.

Maana(fasili) ya lugha inapotajwa mambo yafuatayo huzingatiwa;

(i)          Mfumo maalumu (mpangilio) Lugha lazima iwe na mpangilio maalumu ambao huanzia katika kiwango kidogo kabisa hadi kufikia kiwango cha juu.

(ii)        Sauti za nasibu (sauti za bahati tu), Mara nyingi hakuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya jina la kitu na kile kinachotajwa (kitu)pia hakuna kikao maalum kilichokaa ili kuchagua maneno ya lugha husika na maana zake.

(iii)      Maana- Lugha lazima iwe na maana kwa jamii inayoitumia

(iv)       Binadamu (jamii) – Lugha ni mali ya binadamu, binadamu pekee ndiye hutumia lugha.

(v)         Mawasiliano – Lugha ni chombo cha kupashana habari

 

Vipashio vya lugha

Vipashio vya lugha ni vipengele ambavyo kwa pamoja huijenga lugha. Lugha huundwa na vipashio vikuu vinne ambavyo ni sauti, silabi, neno na sentensi.

 

(a)Sauti

 Sauti ni sehemu ndogo sana ya neno ambayo haiwezi kugawanyika zaidi. Kila lugha ina vitamkwa (sauti) vyake. Sauti zinazotumika katika lugha ya Kichina zinatofautiana na sauti zinazotumika katika lugha nyingine kama vile Kiingereza, Kijerumani, Kiswahili na kadhalika.

Mfano a, b, c,d,e,f,gh,h,I,j,k,l,m,n,nk.

Sauti za lugha ya Kiswahili hugawanyika katika aina mbili ambazo ni irabu na konsonanti.

(i)Irabu/vokali(I)

Irabu ni sauti ambazo wakati wa utamkaji wake huwa hakuna kizuizi katika mkondo wa hewa utokao mapafuni na kupitia mdomoni. Kuna irabu tano za Kiswahili ambazo ni a, e, i, o, u

(ii)Konsonanti(k)

Konsonanti ni sauti ambazo wakati wa utamkaji wake huwa na kizuizi katika mkondo wa hewa utokao mapafuni na kupitia mdomoni.Kuna konsonanti kumi na tisa(19) katika lugha ya kiswahili ambazo ni b,ch,d,f,g,h,j,k,l,m,n,p,r,s,t,v,w,y na z

    Katika lugha ya Kiswahili kwa mfano neno “anacheza” limejengwa kwa vitamkwa a/n/a/ch/e/z/a. Vitamkwa au vipande- sauti hivyo ndivyo vinavyounda maneno.

    Kumbuka kwamba mawasiliano ya kutumia ishara si lugha. Vilevile mawasiliano baina ya wanyama, ndege na wadudu hayawezi kuitwa lugha kwa sababu vitamkwa vyake haviwezi kujulikana wala kuleta maana.

 

 

(b)Silabi                                                     

Silabi ni kipashio kidogo kinachojenga lugha ambacho hutamkwa mara moja na kwa pamoja kama fungu moja la sauti. Silabi inapoungana na silabi nyingine huunda neno.

     Miundo ya silabi

Silabi huweza kujitokeza katika miundo ifuatayo;

·        Irabu pekee(I)
Mfano; Oa, Ua.Hapa kuna silabi mbili kwa kila neno yaani o-a,u-a

·        Konsonanti pekee(K)

Mfano;M-toto,M-kungu

·        Konsonanti na irabu (KI)

Mfano; Baba, Karatasi.Hapa kuna ba-ba,ka-ra-ta-si

·        Konsonanti, konsonanti na irabu (KKI)

Mfano; Mwezi, Chafya.Hapa kuna mwe-zi,cha-fya.

·        Konsonanti, konsonanti, konsonanti na irabu (KKKI)

Mfano; mkwe, pendwa, Mchwa.Hapa kuna m-kwe,pe-ndwa,m-chwa
Kumbuka kuwa silabi ni kipashio cha kimatamshi na hivyo hudhihirika katika matamshi tu.Hivyo basi ili kujua neno lina silabi ngapi unapaswa kulitamka kwanza;kila pigo(fungu) moja la sauti ni silabi moja.

 

 

(c)Neno

Neno ni kipashio kidogo kinachojenga lugha ambacho hutokana na muunganiko wa silabi mbili au zaidi na unaoleta maana kamili.
Mfano; Mama, Lima, Cheza, Cheka.

(d)Sentensi.

Sentensi ni kipashio kikubwa kabisa kinachojenga lugha ambacho kina muundo wa kiima na kiarifu na chenye kutoa taarifa kamili. Sentensi huweza kuwa na neno moja au kikundi cha maneno kinachotoa taarifa kamili.

Mfano;

Ninakuja.
Mama anapika.
Shangazi anashona kitenge.

Tafakuri

1.  Kwa nini mawasiliano ya wanyama, ndege na wadudu siyo lugha?

Jibu lako linaweza kuwa kama ifuatavyo:

i)            Wanyama, ndege na wadudu hawana lugha.

ii)          Lugha ni mali ya binadamu kutokana na sauti zinavyopangiliwa vizuri hata kuleta maana inayojitosheleza.

iii)        Kwa kuzingatia sauti za wanyama tunaona kwamba ni sauti tu zinazoashiria kitu fulani.

iv)         Mnyama anasikia sauti, anaweza pia akaelewa inaashiria nini.

Kazi 1.1

1.  Soma kifungu cha habari kifuatacho kisha ujibu maswali yanayofuata.

 

        Maalufu nchini mwandishi Tanzania Emmanuel Mihambo amejikita katika utunzi wa vitabu vya mapenzi, vitabu ambavyo wanawake wengi Tanzania wa huvisoma muda yote. Wengi hujikutaga wamerara usingizi wakivisoma. Ni kweri hivi vitabu ni motomoto kwani ndani zake zina ujumbe mzito wenye wito wa kujenga hamani na umoja nchini.

        Umaalufu wake mwandishi huyu umevuka mpaka badara ya kuandika kitabu chake cha “nani nimuoe” na ile cha “Nauzika moyo wangu” kinachothimulia namna alivyowahi kukutana na mlembo wa kitanga Tanzania huko.

 

Maswali

i)            Bainisha maneno yenye makosa na uyaandika kwa usahihi

ii)          Kwa nini mwandishi ametumia maneno maalufu, kweri, kurara, badara na thimulia?

iii)        Andika sentensi tatu zenye makosa ya kisarufi yanayotokana na athari za mazingira.

2.  Fafanua tofauti ya irabu na konsonanti kwa mifano

3.  Baada ya Tobi kuzaliwa na mama yake alitupwa katika msitu mnene ambako kulikuwa na sauti za ndege pamoja na wanyama wa mwituni. Akalelewa na nyani mpaka alipofikisha miaka kumi na mitano. Unafikiri Tobi alikuwa akitumia lugha gani baada ya kurejea nyumbani kwao?

Sifa za Lugha/nduni za lugha
Lugha ina sifa mbalimbali ambazo huitofautisha na njia nyingine za mawasiliano.

(i)Lugha huzaliwa,hukua na hufa.

   Lugha ina tabia ya uhai kwani huzaliwa kwa kuanza kutumi
   wa na kikundi kidogo cha watu baadae hukua kwa kupata
   mashiko na kuenea kwenye eneo pana zaidi na baadaye ina
   weza kufa kwa kukosa watumiaji.

 

 

 

Dhima za lugha katika mawasiliano

 

Lugha ina dhima(kazi) nyingi katika jamii. Baadhi ya dhima hizi ni kama ifuatavyo:

(i)          Lugha ni chombo cha mawasiliano

Lugha kama chombo cha mawasiliano humwezesha binadamu kumpatia mwenzake mawazo mbalimbali. Mawazo hayo humfikia binadamu kwa njia ya lugha. Lugha huwawezesha binadamu kufahamiana na kuelewana. Kutokana na kuwasiliana huko umoja na ushirikiano baina ya wazungumzaji huimarika sana. Watu wanaotumia lugha moja hujisikia kuwa ni wamoja ukilinganisha na watu wanaotumia lugha tofauti.

 

(ii)        Lugha ni chombo cha kuelimisha

Sehemu kubwa ya maarifa anayoyapata binadamu hupitia katika lugha. Lugha inatumika kuelezea mambo yanayofaa kufanywa na yale ambayo hayafai kufanywa katika jamii zetu. Watoto wanaozaliwa hujifunza kwa kuyasikiliza yale yanayosemwa.

(iii)     Lugha ni kielelezo cha utamaduni wetu

Mila na desturi na mienendo ya matukio mbalimbali katika jamii yanaenezwa na lugha. Kwa mfano, Kisukuma kinasambaza utamaduni wa wasukuma yaani mila na destri na mienendo yao katika matukio mbalimbali. Mfano wanawake kupiga magoti wakati wa kusalimia au kuweka chakula watu wale. Hivyo hivyo Kiswahili hueneza utamaduni wa watanzania.

(iv)      Lugha husaidia kuhifadhi ujuzi wa ulimwengu na kurithisha ujuzi huo kutoka kizazi hadi kizazi.

Hii ni kutokana na Kiswahili kuenea katika mataifa mbalimbali duniani pamoja na nchi zinazotumia lugha ya Kiswahili zikiwemo Kenya, Uganda, Kongo na Msumbiji.Hivyo kupitia Kiswahili jamii inaweza kuhifadhi maarifa mbalimbali na kuyaeneza kwenye vizazi vijavyo.

 

(v)         Lugha ni chombo kinachoathiri mawazo

Mpangilio wa mawazo hutegemea lugha. Mtu anayefahamu lugha fulani ana nafasi kubwa ya kujieleza au kutoa mawazo yake popote akaeleweka kuliko yule asiyefahamu lugha hiyo.

(vi)      Lugha hupatanisha au kufarakanisha

Lugha hupatanisha kwani husaidia katika kutatua matatizo mbalimbali yaliyomo katika jamii. Hata hivyo lugha inaweza kufarakanisha watu hasa pale unapotokea mgogoro katika jamii na lugha ikashindwa kuutatua mgogoro huo.

(vii)    Lugha hutambulisha matabaka katika jamii

Katika jamii moja unaweza kutofautisha wasomi na wasiosoma kupitia lugha.

  

Tanzu za Lugha

Tunaweza kupanga tanzu za lugha katika tanzu mbili, nazo ni lugha ya mazungumzo na lugha ya maandishi.


Lugha ya mazungumzo ni lugha inayotolewa(kuwasilishwa) kwa njia ya mazungumzo ya mdomo, ni sehemu ya mawasiliano ambayo hujumuisha mzungumzaji na msikilizaji ambapo mzungumzaji huzungumza na msikilizaji husikiliza

Lugha ya maandishi ni ile inayomwezesha mzungumzaji ajieleze kwa njia ya maandishi. Hivyo, lugha ya maandishi humhusisha mwandishi na msomaji (fanani na hadhira).

Umuhimu wa lugha ya kiswahili

l   Lughga ya kiswaili utumik kufundishia masomo yote katik shule ya msingi na vyuo vya kati. Hii husaidia wanafunzi kuelewa zaidi kutokana na kujifunza kwa lugha rafiki.

l   Lugha ya kiswahili huwaunganisha watu.Mfano Tanzania inazaidi ya makabila 120 lakini makabila yote hunganishwa na lugha moja ya kiswhili katika mawasiliano yao.

l   Lugha ya kiswahili ni lugha rasmi ambayo hutumika katika shughuli rasmi na muhimu katika serikali.

l   Lugha ya kiswahili ni nyenzo ya kutolea maarifa, ujuzi na taaluma mbalimbali

l    Lugha ya kiswahili hutoa fursa za ajira kutokana na kiswahili kutumika nje ya nchi yetu, watanzania hupata fursa za ajira mfano; kwenda kufundisha.

Hadhi ya lugha ya kiswahili kimataifa

l   Lugha  ya kiswahili imepewa  hadhi ya kutumika katika shughuli rasmi za kimataifa

l   Lugha ya kiswahili imeafanikiwa kwa kiwango kikubwa kuleta umoja katika bara la Afrika.

l   Kiswahili kinatumika kama lugha rasmi katika jumuiya  ya maendeleo kusini mwa Afrika ( SADC )  na jumuiya ya Afrika mashariki

l   Lugha ya kiswahili  hutoa  fursa za ajira kimataifa, mfano baadi ya watannzania wenye taaluma ya kiswahili wanapopata ajira nje ya nchi

l   Lugha ya kiswahili ndio lugha pekee inayotumika katika umoja wa  Afrika Sanjari na lugha zingine za kimataifa

 

Zoezi la kikundi

1.  Lugha hujengwa kwa vitamkwa, vifafanue vitamkwa hivyo kwa mifano.

 

Kazi ya nyumbani

Binadamu wangeishi bila lugha nini kingetokea? Orodhesha mambo matano ambayo yangetokea.

Nyanja za Lugha

Lugha ya Kiswahili ina nyanja kuu mbili ambazo ni sarufi na fasihi.

Fasihi ni nyanja ya lugha ambayo hutumia maneno kwa njia ya kiufundi (kisanaa) ili kufikisha ujumbe kwa hadhira iliyokusudiwa.

Sarufi ni kanuni na taratibu za lugha zinazofuatwa na wazungumzaji katika mawasiliano. Hivyo sarufi ni kanuni au taratibu zinazotawala matumizi ya lugha.

Kwa hiyo sarufi ya lugha inaweza kugawanyika katika sehemu zifuatazo:

(i)          Sarufi matamshi (fonolojia) vitamkwa vya msingi

(ii)        Sarufi maumbo (mofolojia) mpangilio wa vitamkwa

(iii)      Sarufi muundo (sintaksia) mpangilio wa maneno

(iv)       Sarufi maana (semantiki) upatikanaji wa maana.

Sarufi matamshi (fonolojia)

Sarufi matamshi ni aina ya sarufi inayochunguza namna neno linavyotamkwa. Matamshi ya binadamu yanakumbwa na matatizo kutokana na sababu kuu mbili ambazo ni:

(i)          Athari ya lugha mama

(ii)        Matatizo katika mfumo sauti

Kuathirika huku husababisha kukosekana kwa baadhi ya herufi.

Matatizo haya husababisha kukosekana kwa baadhi ya maana ya moja kwa moja.

Utaratibu wa mpangilio wa vitamkwa vya msingi vinavyojenga maneno hujitokeza katika lugha zote. Tawi hili la sarufi hushughulikia vipande sauti vijengavyo maneno. Vipande sauti hivi ni vidogo vidogo, hivyo haviwezekani kugawanywa zaidi vikaleta maana. Vipande sauti hivyo vinaweza vikaleta tofauti katika maana ya maneno hasa vinapoathiriwa na lugha nyingine.

Kwa mfano;

(i)          Niletee fiatu fyangu – badala ya Niletee viatu vyangu.

(ii)        Wewe metenda zambi – badala ya wewe umetenda dhambi

(iii)      Watoto wamerara kitandani- badala ya Watoto wamelala kitandani

(iv)       Abbas Ibrahim amenunua thamani za ndani – badala ya Abbas Ibrahim amenunua samani za ndani.

Sarufi maumbo (mofolojia)

Ni sarufi inayohusika na namna maneno yanavyoumbika. Huzingatia vipande sauti (vitamkwa) au vipashio vinavyounda neno. Kila kipashio kina kazi yake katika neno.

Kwa mfano,

(i)          Mama atapika

(ii)        Humphrey Lema anafundisha wenzake darasani.

Vipashio na na ta vinatoa maana tofauti ya sentensi, ta inaashiria wakati ujao na na inaashiria wakati uliopo.

Sarufi muundo (sintaksia)

Ni sarufi inayoshughulikia namna maneno yanavyopangwa ili kujenga sentensi. Mpangilio wa maneno katika tungo unaweza kufanya tungo itoe taarifa iliyokusudiwa, au ipotoshe taartifa, au itoe taarifa zaidi ya moja na kumchanganya msikilizaji.

Kwa mfano;

(i)          Kiti mimi nina

(ii)        Mimi nina kiti

Sentensi ya kwanza haieleweki kwa sababu maneno yake hayakupangwa kwa muundo sahihi wa sentensi za Kiswahili.

Sarufi maana (semantiki)

Ni sarufi inayofafanua maana za maneno ya lugha fulani. Pia huzingatia muktadha wa neno linalotumiwa.

Kwa mfano

(i)          Niletee kanga haraka

(ii)        Ukifuata barabara utakuwa salama

(i)          Msikilizaji anayejua ya kuwa kanga ni ndege tu anaweza kumleta ndege huyo, kumbe mzungumzaji amekusudia kuletewa nguo.

(ii)        Mtu asiyejua kuwa barabara ina maana ya sawasawa anaweza kufuata njia anayoiona kuelekea sehemu fulani.

Dhana ya Utamaduni

Utamaduni ni mfumo wea maisha ya watu jinsi wanavyoishi na maandeleo yao kijamiii, kiuchumi, kisiasa, n.k . Tanzania ni moja kati ya nchi zinazosifika duniani kwa kulinda maadili yao

Kuna makabila kama yasiyopungua 120 amabayo yote hutunza mila na desturi zao kwa kiasi tofauti tofauti. Mavazi, salamu na vyakula  ni miongoni mwa mambo yanayobainisha utamadumi wa mtanzania

Lugha ya kiswahili kama kielelezo cha utamaduni wa mtanzania

Matumizi ya lugha ya kiswahili kama kielelezo cha utamaduni wa mtanzania  huweza ujizidhilisha katika misingi ifuatayo;

a)    Lugha nji njia kuu ya mawasiliano na hubadilika kadri jamii inavyobadilika. Ni sehemu ya utamaduni, ni amali ya jamii  ianyoizungumza  na ina alama ya umoja wa taifa. Pia lugha ni utambuylisho wa jamii  na kwa kutumia lugha watu hupashana habari, hujenga uhusiano wa kufahamiana, kuelimishana n kupatana au kufarakana. Bila lugha ingekuwa vigumu  kuurithisha utamaduni wa kizazi kimoja hadi kizazi kingin. Kama lugha itaendele kuwa kielelezo cha utamaduni wa watanzania, basi kiswahili kitaendelea kuwa njia kuu ya mawasilianao ya wanajamii wa watanzania  na hata nje 

b)    Matumizi ya kiswahili katika shughuli za utamaduni yamechochea maendeleo ya jamii ya tanzania kwa namna nyingi.Lugha ya kiswahili hutumiwa na vikundi vya sanaa au vyama mbalimbali vya utamaduni kuwasilisha ujumbe uliokusudiwa.Sanaa za kuchonga kama vinyago pamoja na kwamba zinahitaji kujieleza kwa kuzitazama tu. Lugha ya kiswahili hutumika kutolea ufafanuzi wa fikra mficho katika sanaa  hizo   

c)    Matumizi ya kiswahili hudhihirika katika nyimbo ambazo huwa na mafunzo na maadili fulani kwa jamii kwa mfano; maadili ya kuwaelimisha wanajamii kuhusu mambo mbalimbali

d)    Katika magazeti na vyombo vingine vya habari,Lugha ya kiswahili ni mojawapo ya lugha zinazotumika kuelezea, kuelimisha na nakuburudisha wanajamii kuhusu mambo kadhaa  wa kadhaa yakiwemo ya  utamaduni.Michoro ya vikatuni kuambana na maelezo yaliyoandikwa kwa lugha ya  kiswahili ili kutoa mafunzo mbalimbali ya kitanzania  kwa walengwa

e)     Viongozi wa dini hutumia lugha ya kiswahili katika kutunga sheria na kanuni pamoja na kuandika vitabu  vyenye mambo bora ya kuelimisha jamii

 

Umuhimu wa kulinda na kuhifadhi utamaduni wa kitanzania

 

a)    Kutambua na kulinda rasilimali , mazingira na urithi wa                         utamaduni

b)    Kuhakikisha na kuhimiza usawa katika matumizi bora ya          mgawanyo wa haki na rasilimali na miliki

c)    Utamaduni husaidia  kuenzi na kutunza  tabia njema  na kukemea vitendo viovu  kama vile matumizi matumizi ya dawa za kulevya , ulevi , wivu, uzembe n.k

d)    Utamaduni husaidia kutambua na kuthamini kazi halali  kuwa ni msingi wa maisha na maendeleo ya binadamu

e)    Utamaduni husaidia kuiandaa jamii kutambua kwamba, elimu, mafunzo na ubunifu  ni muhimu katika kuzalisha mali nna kuendesha mambo ili kuongeza tija na kuleta ufanisi

f)      Utamaduni husaidia kuinua hali ya maisha ya jamii  kupitia nguzo zake kuu mfano sanaa za ufundi na sanaa za maonyesho   

g)    Utamanuni au jamii  kuthamini na kutumia ujuzi, taaluma na teknolojia ya kisasa na ya jadi kuimarisha afya, matumizi bora ya mazingira, rasilimali na kuendeleza jamii

h)   Uta,maduni hujenga tabia ya ushirikiano, mshikamano, udugu, uzalendo, upemdo na moyo wa kuvumiliana wakati wa shida na raha

i)      Utamaduni  hulitambulisha na kulingaza taifa nje ya mipaka yake na kuimarisha uhusiano wa kitaifa.

 

 

Kuwasiliana kwa njia ya mazungumzo

Dhana ya Mazungumzo.

Mazungumzo ni utaratibu wa kuongea baina ya pande mbili ambapo wahusika wa mazungumzo hayo huwa ni watu. Kwa kawaida mazungumzo huwasilishwa kwa njia ya mdomo na huweza kuambatana na ishara za viungo vya mwili. Chanzo cha mazungumzo huwa ni mzungumzaji na kikomo chake huwa ni msikilizaji.

Mzungumzaji huwa ni mtu anayeanzisha uneni, huyu kifasihi huitwa fanani. Uneni ni utoaji wa matamko yenye maana katika lugha fulani ilihali kitendo ni dhana ya utendaji . Msikilizaji huwa ni mtu anayepokea uneni kutoka kwa mzungumzaji huyu kifasihi huitwa hadhira.

Misingi ya Mazungumzo

Ili watu waweze kuelewana vizuri wanapozungumza ni lazima wazingatie mambo makuu yafuatayo,Pia mambo hayo yasipozingatiwa yanaweza kuathiri mazungumzo ya wazungumzaj

(i)           Uhusiano wa wazungumzaji

Unaweza kuelewa na kutambua uhusiano wa watu wanaozungumza kama ni marafiki , wapenzi, baba na mtoto au mwalimu na mwanafunzi watu au wazungumzaji ni maadui kwa kuangalia msamiati wanayotumia katika mazungumzo yao. Msamiati wanayotumia katika mazungumzo yao. Msamiati anayotumia mwalimu na mwanafunzi wake ni tofauti sana na msamiati anayotumia mtoto na wazazi wake kwa sababu , msamiati utakaotumika na mwalimu na mwanafunzi  wake hutawaliwa na heshima busara na ulezi zaidi tofauti na msamiati utakaotumika na mtoto na wazazi wake kwani yenyewe hatawaliwa na madoido, madokezo na mabembelezo zaidi.

(ii)         Mada inayozungumzwa

Mazungumzo hutawaliwa na mada , mazunguzumo huhusisha mada inayozungumzwa ambayo pia huamua msamiati kwa kutumia katika mazungumzo husika. Kwa mfano mada inaweza kuwa siasa, masomo, sherehe au muziki. Wazungumziaji wana takiwa kuchagua msamiati kulingana na mada. Kwa mfano mada ya masomo inaweza kuibua msamiati kama vile elimu, itifaki.

(iii)       Muktadha wa Mazungumzo

Mazungumzo huathiriwa na miktadha tofauti tofauti muktadha wa mazungumzo unaweza kuwa rasmi au usiwe rasmi, kuna miktadha mbalimbali ambayo wazungumziaji huweza kutumia wakati wa mazungumzo yao. Miktadha kama hiyo ni shuleni, dukani, mjini, barabarani, kijijini n.k . Kwa mfano , lugha anayotumia daktari hospitalini ni tofauti na lugha anayotumia daktari huyohuyo akiwa nyumbani kwake hivyo lugha hutofautisha kulingana na muktadha wazungumzaji wanapaswa kuzingatia muktadha wa mazungumzo yao.

Mfano.

Mazungumzo ya mama na mwanae wakiwa kwenye daladala.

MTOTO:Mama , mbona kila siku baba anakupiga?

MAMA:Chukua andazi mwanangu.

 

Kwa mfano huu, Mama amezingatia muktadha ndio maana hahitaji mazungumzo yaendelee , kwani mada husika haifai kuzungumziwa kwenye daladala

(iv)        Lengo la mazungumzo

Mzungumzaji huwa na lengo la kuzungumza anapokutana na mwenzake ili kukidhi lengo la mazungumzo, mzungumzaji huhitaji kutoa ufafanuzi wa yale anayoyasema ili msikilizaji aelewe kama ilivyokusudiwa . Lengo la mazungumzo linaweza kuwa kutoa taarifa , kuhoji, kukejeli ,kuelimisha ,kuonya au kutia moyo.

(v)          Muda /wakati wa mazungumzo

Mzungumzaji ni lazima ateue msamiati utakaoendana na wakati katika eneo husika . Matumizi mabaya ya muda katika eneo amabalo si rafiki hufanya mazungumzo kuchosha.

(vi)        Utanzu au aina ya mawasiliano

Kabla ya mazungumzo , mzungumziaji ni lazima ajiulize kwamba ujumbe aliokusudia kufikisha kwa hadhira ataufikisha kwa mbinu ipi? Mbinu ya majadiliano, masimulizi, hotuba au nyimbo.

(vii)      Shughuli inayofanyika

Msamiati unaotumika katika mazungumzo huendana na shughuli inayohusika kwa mfano kama shughuli inayofanyika ni ufugaji , uchimbaji madini na msamiati wake utaendana na shughuli husika.

Mifano ifuatayo inaonesha mazungumzo katika miktadha tofauti.

Mfano 1 Mazungumzo ya kanisani

 

MCHUNGAJI: Bwana Yesu apewe sifa

WAUMINI: Amina

MCHUNGAJI: Naomba mfungue biblia zenu.

 

Mfano 2 Mazungumzo ya marafiki.

 

BAHATI: Mambo sanura?

SANURA: Poa tu vipi wewe?

BAHATI :Fresh rafiki yangu, vipi jana mama hakukutia ndimu ulipochelewa kurudi?

SANURA: Loo! Mama Yule na ule mdomo wake, alinichimba biti sana.

 

Mfano 3. Mazungumzo ya shuleni

 

MWANAFUNZI:Shikamoo mwalimu

MWALIMU: Marahaba , hujambo?

MWANAFUNZI: Sijambo

 

 

(viii)    Hali za wahusika wakati wa mazungumzo

Lugha inayotumika inapaswa kuendana na hali za wahusika wakati wa mazungumzo ili kuleta maelewano . kwa mfano kama mzungumzaji ni mgonjwa au amekasirika, lugha inayotumika kuwasiliana naye itaendana na hali hiyo.

Andaa mazungumzo yanayoweza kuzungumzwa katika maeneo yafuatayo;

a)     Hospitalini

b)     stendi ya mabasi

c)     Dukani

d)     Sokoni

e)     Shuleni

 
ZOEZI

 

 

 

 

 

 

Hatua za kufanya mazungumzo katika lugha ya kiswahiliKatika kufanya mazungumzo zipo hatua mbalimbali za kufuata wazungumzaji wanapokutana kuzungumza , Hatua hizo ni hizi zifuatazo;

Salamu

Watu wawili wanapokutana kuzungumza sharti wasalimiane kabla ya kuanza mazungumzo hayo, Jambo la kwanza huwa ni salamu, salamu hii huwa rasmi au isiyo rasmi kutegemea na uhusiano uliopo baina ya wazungumzaji , Salamu rasmi inaweza kuwa kama ifuatavyo; Habari za asubuhi na habari za kazi, Salamu zisizo rasmi inaweza kuwa hujambo? Mambo, vipi hali yako, kumbuka kuwa “kwa heri “ siyo salamu.

Utambulisho

Wazungumzaji wanapokutana wana nafasi ya kutambuana . kipengele hiki hufanyika mara baada ya wahusika kusalimiana katika utambulisho wazungumzaji hutaja majina yao na wasifu wao kwa ujumla. Kwa mfano, unaitwa nani, wewe ni nani?. Hii huwasaidia wazungumzaji kujenga mipaka, uhusiano na mazoea , ukimtambua mtu unayezungumza naye itakupa urahisi wa kuchagua msamiati utakaotumia unapozungumza naye.

 

Mazungumzo mafupi

Mara baada ya utambulisho , wazungumzaji hufanya mazungumzo mafupi kwa nia ya kutaka dhima ya mazungumzo yao.

Mazungumzo kamili

Mazungumzo kamili hutegemea muktadha, lengo la mazungumzo , mada ya mazungmzo na uhusiano uliopo baina ya wazungumzaji . Ni sehemu hii ambayo hutumia muda mrefu wakati wa mazungumzo.

 

Ufafanuzi

Ni kipengele kinachohusu mambo yote ambayo hayakueleweka kwa mmoja kati ya wazungumzaji ,hivyo kurudiwa na kutolewa maelezo ya ziada.

Kukatisha Mazungumzo

Kipengele hiki ni muhimu sana wakati wa mazungumzo, mathalani umetembelewa na ndugu yako ofisini kwako, kwa bahati mbaya ndugu yako huyo anaongea sana kiasi kwamba wageni wengine wanalalamika nje ya ofisi inakupasa ukatishe mazungumzo . zipo njia mbalimbali za kukatisha mazungumzo mfano, kama umekaa kwenye kiti unaweza kusimama kisha kumsogelea na kumpa mkono mtu unayezungumza naye ukaongea naye kwa maneno kama vile “Nitakushukuru, karibu tena, tuonane wakati mwingine n.k

Kuagana

Tumia maneno kulingana na muktadha mfano kama ni ofisini waweza kutumia maneno rasmi kama vile “Nakutakia kazi njema, kila la kheri , tuonane wakati mwingine na unaweza kutumia maneno kama vile baadaye furahia siku yako katika muktadha usio rasmi.

 

 

Lugha fasaha

Lugha fasaha ni ile ambayo inafuata taratibu zote za lugha hiyo ikizingatia maana, matamshi, muundo na mantiki. Lugha inapotumika vibaya huweza kupotosha lengo la mzungumzaji. Makosa haya yanaweza kujitokeza katika msamiati (maana) miundo, matamshi na mantiki. Kwa mfano, Kurara, neno hili si neno fasaha kwa sababu katika lugha ya Kiswahili hutamkwa kulala. Ili mazungumzo yaweze kuwa mazuri, wazungumzaji lazima watumie lugha kwa ufasaha. Angalia makosa mbalimbali ambayo huweza kufanywa na watumiaji wa lugha fasaha katika misingi ya maana, miundo, matamshi, kuacha baadhi ya maneno, kuongeza vitamkwa au silabi, makosa katika matumizi ya nyakati na mantiki.

 

(i)           Makosa ya kimaana / Kimsamiati

Ili lugha iwe fasaha ni sharti neno lililokusudiwa liwe fasaha. Kuna maneno mengi yenye maana zaidi ya moja. Maneno haya ni kama vile, kaa, kata, chungu, mbuzi, kanga, barabara, panda, susa, kanda.

Tazama namna maneno haya yanavyoweza kuleta dhana nyingine:

§  Susa -        Tikisa mti

-           Uchafu utokanao na mabaki ya chakula

-           Kataa kufanya jambo

-           Sehemu ya muwa isiyo tamu

 

§  Kata -        Eneo la kijiografia

-           Gawanyisha kitu katika vipande

-           Chezesha viungo vya mwili kama vile macho,kiuno shingo.

Hapa ndipo maneno kuwakilisha badala ya kuwasilisha, baada badala ya badala hufafanuliwa.

Mfano

l   Mvu imepiga sana usiku  badala ya mvua imenyesha sana usiku

l   Mwalimu alidondoka mlangoni badala ya mwalimu alianguka mlangoni

l   Spika alimwasilisha Rais badala ya spika alimwakilisha Rais

l   Ashura amenona sana badala ya Ashura amenenepa sana

l   Ng’ombe amejifungua badala ya ng’ombe amezaa

Baadhi ya maneno ambayo tofauti zake za kimaana zinatofautishwa na mkazo katika jinsi neno linavyotamkwa.

 

(ii)         Makosa ya kimuundo

Mpangilio mzuri wa maneno katika sentensi hufanya lugha kuwa fasaha. Mfuatano wa maneno husaidia kuleta maana iliyokusudiwa. Kwa mfano “Wanaitwa wanafunzi badala ya Wanafunzi wanaitwa”. “Kizinga anaitwa na Juma” badala ya Kizinga na Juma wanaitwa.

 

(iii)       Makosa ya kimatamshi

Matamshi mazuri ya sauti za lugha hujenga ufasaha wa lugha hiyo. Watu wengine hushindwa kutamka baadhi ya sauti za Kiswahili kwa sababu ya athari za lugha mama na athari za kimaumbile, hususani kithembe, kibogoyo na toinyo. wengine huchanganya na kubadili sauti hizo. Mifano ya maneno haya ni kama yafuatayo:

Ÿ  Ngombe badala ya ng’ombe

Ÿ  Mbusi badala ya mbuzi

Ÿ  Kurara badala ya kulala

Ÿ  Zambi badala ya dhambi

Ÿ  Langi badala ya rangi

Ÿ  Zarura badala ya dharura

Ÿ  Ntu badala ya mtu

Ÿ  Thatha badala ya sasa.

(iv)Makosa ya kimuundo
Haya ni makosa ambayo hutokana na kutokuwa na mpangilio mzuri wa maneno katika sentensi.Mara nyingi sentensi za Kiswahili kimuundo huanza na nomino au kiwakilishi,kisha hufuatiwa na kivumishi,hufuata kitenzi na kisha aina nyingine za maneno.Baadhi ya wazungumzaji hushindwa kufuata utaratibu huu na kujikuta wakikosea kama mifano ifuatavyo inavyoonekana;Kiti mimi nina badala ya mimi nina kiti.
   Mama chakula anapika badala ya Mama anapika chakula
(v)Makosa ya kuongeza vitamkwa.
     Ni makosa ambayo hufanywa na watumiaji wa lugha kwa
     kuongeza vitamkwa au silabi katika maneno sehemu
     ambapo hapatakiwi.Mara nyingi makosa kama haya
     husababishwa na athari za lugha mama.
      Mfano;
      Msichana msafi anaitwa badala ya msichana safi anaitwa.
      Mimi nakuambiaga badala ya mimi huwa nakuambia.
      Mashuleni pawe safi badala ya shuleni pawe safi.

(vi)Makosa ya kuacha maneno
      Ni makosa ambayo watumiaji wa lugha huacha kuyatamka au kuyatumia baadhi ya maneno fulani katika sentensi wakiamini kuwa ujumbe walioukusudia utakuwa umefika kwa hadhira.
Mfano,
Baba amerudi kazini badala ya baba amerudi kutoka kazini.

          

(vii)Makosa ya Mantiki

Ni utaratibu mzuri wa kufikiri ili kupata maana iliyolengwa. Kwa mfano:

-      Mfupa hauna ulimi badala ya ulimi hauna mfupa.

-      Chai imeingia nzi badala ya nzi ameingia kwenye chai.

-      Nimemkuta hayupo badala ya sijamkuta.

-      Kitumbua kimeingia mchanga badala ya mchanga umeingia ndani ya kitumbua.

 

Umuhimu wa kutumia lugha kwa ufasaha

·         Hufikisha ujumbe uliokusudiwa kwa urahisi zaidi.

·         Huifanya lugha kuwa na thamani na hadhi kubwa.

·         Huwavutia watu na kuwafanya kujifunza lugha kirahisi.

·         Huifanya lugha ikubalike ndani na nje ya nchi.

·         Huboresha uhusiano wa watumiaji wa lugha husika.

·         Hufanya lugha iwe na mvuto na yenye kushawishi watumiaji wapya.

·         Hudumisha sarufi ya lugha.

·         Hukuza na kuendeleza utamaduni wa jamii.

Athari za kutotumia lugha kwa ufasaha

(i)           Kupata maana ambayo haijakusudiwa.

(ii)          Watumiaji kutoelewana.

(iii)        Lugha kushuka hadhi yake na kuonekana kama ni lugha ya wahuni.

(iv)         Inaweza kuchochea ugomvi baina ya watumiaji kutokana na kutoelewana hasa wakati wa utumiaji wa msamiati.

(v)          Kuondoa umoja na mshikamano kwa sababu tu lugha ndio kiunganishi cha watu hasa wanaoelewana.

 (vi)Hudumaza utamaduni wa jamii.

 (vii)Husababisha ujumbe ushindwe kufika kama ulivyokusudiwa.                                           

 

 

 

Zoezi la mada

1.   Chagua herufi ya jibu sahihi katika vipengele (i) – (v), kisha andika herufi ya jibu hilo katika sehemu ya kujibia.

(i)           Mawasiliano baina ya wanyama, ndege na wadudu hayawezi kuitwa lugha kwa sababu gani?

A.   Vitamkwa vyao ni hafifu

B.   Lugha ni mali ya wanyama tu

C.   Vitamkwa vyao havina maana

D.  Vitamkwa vyao havina irabu

E.   Vitamkwa vyao ni vya msingi katika utamkaji

(ii)          Kanuni maalumu na taratibu za lugha zinazofuatwa na wazungumzaji katika mawasiliano huitwaje?

A.   Lugha    B. Sarufi   C. Lugha fasaha   D. Utumizi wa lugha   E. Mawasiliano

(iii)        Neno abab halikubaliki lakini neno baba linakubalika kwa sababu gani?

A.   Mpangilio wa neno

B.   Mpangilio wa irabu

C.   Mpangilio wa vitamkwa

D.  Mpangilio wa fonimu

E.   Mpangilio wa mofimu

(iv)         Dhima kuu ya lugha katika mawasiliano ni ipi kati ya hizi zifuatazo?

A.   Kutambulisha utamaduni

B.   Kutunza historia

C.   Kupashana habari

D.  Kuelimisha jamii

E.   Kuburudisha jamii

 

 

 

(v)          Zipi ni aina mbili za fonimu katika lugha ya Kiswahili?

A.   Irabu na konsonanti

B.   Irabu na silabi

C.   Irabu na mofimu

D.  Konsonanti na kiambishi

E.   Foni na alofoni

2.   Oanisha dhana zilizopo safu A na mifano yake iliyopo safu B kwa kujaza herufi ya jibu sahihi kwenye safu A.

 

Safu A

Safu B

(i)           Vokali

(ii)          Haitamkiki bila kuwekewa irabu

(iii)        Huundwa kwa sauti ya konsonanti

(iv)         Huundwa na irabu pamoja na konsonanti

(v)          Huunda lugha

A.   Sauti

B.   Neno

C.   Silabi

D.  Konsonanti

E.   Lugha

F.   Mfumo

G.  Nasibu

 

3.   Panga fonimu hizi kwa utaratibu unaofaa ili kujenga neno la Kiswahili.

(a)  Ambit

(b)  Awsa

(c)  Ynmzaa

(d)  Orsdai

(e)  ngzoao

4.   Eleza kwa kifupi dhima kuu tano za lugha

5.   (a)      Fafanua maana ya lugha fasaha

(b)      Fafanua madhara matano (5) ya kutumia lugha isiyo    fasaha

6.   Eleza tofauti baina ya sauti hizi

(a)  /a/ na /p/

(b)  /g/ na /t/

(c)  /f/ na /ng/

(d)  /th/ na /n/

(e)  /w/ na /y/

7.   Eleza maana ya dhana zifuatazo

(i)           Lugha

(ii)          Lugha fasaha

(iii)        Irabu

(iv)         Konsonanti

(v)          Silabi

8.   Sahihisha sentensi zifuatazo

(a)  Doto ameungama zambi zake

(b)  Watoto walirara sakafuni

(c)  Mzee Kapinga anapaka langi nyumba yote

(d)  Masanja amewasili jana kutoka ngambo

(e)  Mbusi hii inapenda kutoroka sana.

9.   Eleza maana mbili za kila neno

(a)  Paa

(b)  Vua

(c)  Panda

(d)  Randa

(e)  Kanda

10. Fafanua mambo ya kuzingatiwa ili kuwezesha mawasiliano katika mazungumzo.

 

Powered by Blogger.

Wasiliana nami papo kwa papo

Name

Email *

Message *

Ads 468x60px

Breaking News

Top Featured

Featured Posts

Sample text

Sample Text

Recomended

Facebook

Advertise

Most Popular

Connect With Us

Followers

Social Icons

Pages

Pages

BTricks

Pages

Popular posts

Tafuta chochote ukiwa hapahapa

Kategori

Recent Comments

You can replace this text by going to "Layout" and then "Page Elements" section. Edit " About "

recent posts

Video Of Day

TRANSLATE

Instructions

Video

Flickr Images

FURAHIA UWEPO WAKO HAPA

Logo Design by FlamingText.com
Logo Design by FlamingText.com

Imetembelewa mara

NUMBER OF VIEWERS

Popular Posts

SAJIRI

Definition List

premium-wordpress-themes.org