Imeandaliwa na Mtila Mswahili.
Ushairi ni mojawapo ya matawi kongwe na muhimu ya fasihi, unaotumia
lugha kwa namna ya kipekee kufikisha hisia, mawazo, na uzoefu wa mwanadamu.
Tangu zamani, ushairi umekuwa chombo cha burudani, elimu, kumbukumbu ya
historia, na hata harakati za kijamii. Katika muktadha wa fasihi ya Kiswahili,
ushairi una nafasi ya kipekee kutokana na utajiri wake wa miundo, matumizi ya
lugha, na uwezo wake wa kuwasilisha ujumbe kwa njia inayovutia na kukumbukwa
kwa urahisi.
Kazi hii inalenga kuchambua kwa kina sifa bainifu za ushairi wa
Kiswahili. Lengo kuu ni kutoa ufahamu wa kina kuhusu vipengele
vinavyoutofautisha ushairi na aina nyingine za maandishi, huku tukiangazia
umuhimu wa kila sifa katika kuunda kazi bora ya kishairi.
Kwa hivyo, kwa kuzingatia sifa bainifu za ushairi ulizotusomesha
darasani, nitazitolea maelezo na mifano madhubuti kwa kila moja kutoka katika
mashairi mbalimbali ya Kiswahili ili kuonyesha jinsi sifa hizi zinavyojitokeza
katika uhalisia wa kazi za sanaa, nikijumuisha marejeo ya kitaaluma niliyo
yasoma ili kuimarisha uhalali wa maelezo haya kama ifuatavyo:
Ushairi hutumia lugha ya
mkato au lugha ya ufupisho.
Ushairi mara nyingi hutumia lugha iliyofupishwa ili kuleta urari wa
mizani na vina, na pia kuongeza ukali na uzito wa ujumbe. Maneno yanaweza
kufupishwa kwa kuacha baadhi ya herufi au silabi. Kwa mfano tukitazama shairi la
"Usafi" lililoandikwa na " Haji Gora Haji " katika shairi
hili anatumia lugha ya mkato ili kufikia urari wa mizani na vina, na pia
kuongeza wepesi katika usomaji.
Mfano:
"Kipindupindu
twajuwa, maradhi yanohiliki
Usafi ni yake
dawa, kufanyiza hatutaki
Hatua ikichukuwa,
serikali twaichuki
Tusiwe kama
mapunda, tukenenda kwa michungo"
Hapa mwandishi ametumia neno "twajua" badala ya
"tunajua"
Ametumia neno "kufanyiza" badala ya " kufanya"
Pia ametumia neno " twaichuki" badala ya
"tunaichukia".
Matumizi ya maneno haya
yanaonyesha jinsi mshairi anavyobadilisha umbo la maneno ili kukidhi mahitaji
ya kimuziki ya shairi. Licha ya ufupisho huu, maana ya maneno inasalia kuwa
wazi
Kwa hivyo matumizi haya ya lugha ya mkato si tu yanafaa katika
kudumisha muundo wa kishairi, bali pia yanaweza kuongeza uhai na wepesi katika
usimulizi au uwasilishaji wa hisia.
Ushairi ni kazi ya kubuni.
Ushairi kwa asili yake ni kazi ya ubunifu. Ingawa unaweza kuakisi
matukio halisi au hisia za kweli, msingi wake ni uwezo wa mshairi kuunda picha,
mawazo, na hisia kwa kutumia lugha kwa njia ya kipekee na ya kisanii.Kwa mfano,
Shairi la " kimbunga" ni kazi ya kubuni inayoonyesha au kuashiria
hisia za kuleta mabadiliko kupitia hali tofauti ili kuleta maendeleo katika
jamii nzima. Mshairi "Haji Gora Haji " anatumia uwezo wake wa
kufikiri na kuhisi kuunda maneno yanayoelezea hali hii kisaikolojia.
Mfano: Mstari "Kimbunga
mji wa siyu, kilichowahikufika" si kauli halisi ya kimwili bali ni ubunifu
wa lugha unaowakilisha hisia kali za kutaka kufanya mabadiliko.
Ubunifu hapa unajidhihirisha katika jinsi mshairi anavyochagua
maneno na kuyaweka katika mtiririko unaoamsha hisia fulani kwa msomaji. Hata
kama hisia zinazoelezwa zinaweza kuwa za kweli, uwasilishaji wake kwa njia ya
kishairi ni zao la ubunifu wa mwandishi.
Kwa mfano shairi la " wewe peke yako" ni shairi ambalo
lipo katika ushairi wa Fungate ya uhuru, mwandishi Mohamed Seif Khatib ameweza
kubuni kazi yake na kuamsha hisia kali za kimahaba na kimapenzi kwa wapendanao
mfano pale aliposema:
"Nilopenda kwako, yametimilia,
Hunaye
mwenzako, anaokufikia,
Wewe peke
yako, nimesharidhia."
Ushairi hutumia lugha na msamiati teule.
Washairi hutumia lugha na msamiati ulioteuliwa kwa uangalifu ili
kufikisha ujumbe wao kwa usahihi, kwa nguvu, na kwa urembo. Uchaguzi wa maneno
huzingatia muktadha, hisia, na athari wanayotaka kuifikia kwa hadhira. Kwa
mfano tukitazama shairi la "Kimbunga", "Haji Gora Haji" anatumia lugha
rahisi lakini yenye nguvu katika shairi hili. Uchaguzi wa maneno kama
"kimbunga," "kibwangai," "nyani" na
"chui" unafanyika kwa uangalifu ili kuwasilisha hisia za uchungu
za kutaka hamasa ya kupambana na mambo
kama ukoloni mamboleo, usaliti, mapinduzi na kadhalika.
Mfano: Neno
"kimbunga" linatoa picha kali ya kutaka mapinduzi ama mabadiliko kwa
mfano pale aliposema:
"Kimbunga mji wa siyu, kilichowahi kufika
Si kwa yule
wala huyu, ilikuwa patashika
Kimeing'owa
mibuyu, minazi kunusurika
Nyoyo
zilifadhaika."
Kwaiyo kupitia ubeti huu mwandishi ametumia neno
"kimbunga" kueleza kuwa jamii ipo haja ya kuondosha dhulma, unyanyasaji na udhalilishaji dhidi ya
wanyonge. Dhulma inapo kithiri ipo haja ya jamii kuungana kufanya mapinduzi ili
kuondosha dhulma hizo.
Aidha neno
"kibwangai" kwa mujibu wa
mwandishi mwenyewe katika shairi hili linaashiria viongozi wasaliti hali inayowasababishia maumivu na mateso ya kihisia wanajamii kwa
kutarajia manufaa bora kwa viongozi wanaowachaguwa kuleta mabadiliko na
maendeleo bora katika jamii zao, lakini wanapoyapata madaraka huwasahau na huwa
hawajali kuwa wana deni kwa wananchi wao.
Kwa mfano pale aliposema:
"Kibwangai lipoona, ni mtu kakamiliya
Akaanza
kujivuna, na dharau kuzidiya
Wala hakujali tena, wenzake
walomwambia
Akahisi
hawi nyani, umbile lile litadumu.
"Kawa na tabia moja, nyani walipomwendeya
Akajifunga mkaja, mijiwe kuwarushia
Hakujali
zao haja, wala kuwahurumiya
Kupiga na kukemeya, pia na kuwashutumu."
Mfano mwengine: Badala ya kusema "ana huzuni sana,"
mshairi anaweza kutumia maneno kama "moyo wake umejaa simanzi nzito"
au "roho yake inavuja damu ya majonzi."
Msamiati teule hapa unalenga kuamsha hisia fulani kwa msomaji na
kuwasilisha ujumbe kwa njia inayoeleweka na yenye nguvu. Licha ya unyenyekevu
wa maneno, yana uzito mkubwa wa kihisia.
Ushairi hutumia lugha za kitamathali za usemi.
Tamathali za usemi ni matumizi ya lugha kwa njia isiyo ya kawaida
au ya moja kwa moja ili kuleta maana nyingine, kusisitiza jambo, au kuunda
picha hai akilini mwa msikilizaji au msomaji.
Mifano: kupitia uhairi
wa "Fungate ya uhuru" mwandishi
"Mohamed Seif Khatib" ameweza kutumia lugha za kitamathali za usemi kupitia mashairi
mbalimbali kama ifuatavyo:
Tashbiha
Katika shairi la "Mkata" lililokuwepo katika mashairi ya
Fungate tumeweza kuona mfano wa tashbiha ufuatao:
" kibandani,
nilalapo, kama dema la samaki,
Samaki nimo
demani,
................................................"
Hivyo mwandishi ametumia tamathali hii lengo lake haswa ni
kutuonesha maisha halisi na tatizo la umaskini kwa baadhi ya watu katika jamii.
Sitiari
Kupitia shairi la "Uwapi uzuri wako" mwandishi " Mohamed Seif Khatib ameweza
kutuonyesha sitiari ambayo imebeba maana nzito na mafunzo makubwa kwa
jamii katika shairi hili.Mfano pale
aliposema:
"Sasa
jamvi la wageni, wajapo huwapokea,
Imekutoka thamani, mtu duni mebakia,
Hata mbwa wa
mjini, kikuona hukimbia,
Uwapi uzuri
wako, ya wapi Maringo yako".
Katika mshororo wa mwanzo ndipo ilipo sitiari, ambayo mwandishi
ameitoa hapo kwa lengo hasa ili kutuonyesha suala au tatizo kubwa la ukahaba
hasa kwa akina dada zetu katika jamii zetu kwasababu ni janga kubwa hili na
lina madhara kwa taifa letu. hivyo basi, anawatanabahisha kuachana na suala
hilo.
Tafsida
Tafsida katika shairi la Paka shume" ambalo pia ni miongoni
katika mashairi yaliyopo katika kitabu cha ushairi wa "Fungate ya
Uhuru", Mohamed Seif Khatib anatoa onyo kali, lakini anafanya hivyo kwa
lugha ya kishairi na yenye hekima, ambayo inaweza kuonekana kama aina ya
tafsida kwa mfano pale aliposema:
"Paka mtaka vya watu,
itakufika ajali,
Watambaa
kama chatu, nyumbani kwa bwana Ali,
Kwake
hutopata kitu, kwani mwenyewe mkali."
Lengo hasa la mwandishi kupitia ubeti wa shairi hili ni
kutanabahisha jamii kuhusu heshima kwa binti wa watu, lakini pia ni jambo zuri
kuheshimu ndoa za watu katika jamii ili kuepuka kupata hatari iliyoelezwa na
mwandishi.
Kwa hivyo, matumizi ya tamathali za usemi huongeza urembo, kina, na
nguvu ya hisia katika ushairi, na kumfanya msikilizaji au msomaji ahusike zaidi
na ujumbe.
Ushairi huwasilishwa mbele ya hadhira.
Kiasili, ushairi mwingi ulikuwa na lengo la kuwasilishwa kwa
hadhira, iwe kwa kukaririwa, kuimbwa, au kuchezwa. Hata ushairi ulioandikwa una
nguvu yake inaposomeka kwa sauti au kuigizwa mbele ya watu.
Mfano: Mashairi ya Kiswahili
ya kale kama vile Utenzi wa Tambuka na Utenzi wa Fumo Liyongo yalikuwa
yakisimuliwa na kuimbwa mbele ya jamii.
Uwasilishaji mbele ya hadhira huwezesha mshairi au muwasilishaji
kuwasiliana moja kwa moja na wasikilizaji, kuona miitikio yao, na kuongeza
nguvu ya ujumbe kupitia toni ya sauti, ishara, na mwingiliano.
Muasilishaji wa ushairi anaweza kuwa mtu mmoja.
Ingawa kuna aina za ushairi zinazohusisha uimbaji au uwasilishaji
wa kikundi, mara nyingi ushairi huwasilishwa na mtu mmoja ambaye ni mshairi
mwenyewe au mtunzi aliyejifunza kazi hiyo.
Mfano: Katika mashindano ya
ushairi (slam poetry), kwa kawaida mshairi mmoja husimama mbele ya hadhira na
kuwasilisha kazi yake.
Kwa hiyo, uwasilishaji wa mtu
mmoja humpa nafasi ya kuonyesha uwezo wake binafsi wa kisanii, ufasaha wa
lugha, na uwezo wa kuhuisha maneno na hisia za shairi.
Ushairi huwa na muundo
maalum.
Ushairi kwa kawaida huwa na muundo uliopangwa, ambao unaweza
kujumuisha idadi maalum ya mistari (beti), urari wa mizani (idadi ya silabi
katika kila mstari), na mpangilio wa vina (sauti zinazofanana mwishoni mwa
mistari).
Mfano: kwa kuangalia ushairi wa "Nia yangu
sigeuzi " mwandishi "Mohamed Seif Khatib ametumia muundo ufuatao:
"Rabi
utubarikie, la wawili pendo letu,
Rehemu
tuzidishie, zisafishe nyoyo zetu,
Roho zetu
zitulie, tusitamani vya watu."
Uchambuzi wa Muundo katika ubeti huu ni :
Idadi Maalum ya Mistari:
Mwandishi katika ubeti huu
ametumia muundo kwa kizingatia idadi ya mistari , ambapo ametumia muundo wa
Tathlitha amabao shairi huundwa kwa mistari mitatu.
Urari wa Mizani:
Urari wa mizani unahusu
idadi ya silabi katika kila mshororo. Katika ubeti huu, tunaona kuwa idadi ya
mizani inalingana kwa mishororo yote: ambapo:
Mshororo wa kwanza: Una mizani 16
"Ra-bi-u-tu-ba-ri-ki-e =( 8) "la-wa-wi-li-pe-ndo-le-tu"
(8) =16
Mshororo wa pili: "
una miazani 16
"Re-he-mu-tu-zi-di-shi-e (8), zi-sa-fi-ke-nyo-yo-ze-tu (8)= 16
Mshororo wa tatu: una mizani 16
"Ro-ho-ze-tu-zi-tu-li-e (8), tu-si-ta-ma-ni-vya-wa-tu (8) =16
Mpangilio wa Vina:
Tunaangalia maneno yanayoishia katika kila mstari:
Mstari wa kwanza unaishia
na: -tu
Mstari wa pili unaishia na:
-tu
Mstari wa tatu unaishia na:
-tu
Mpangilio wa vina katika ubeti huu ni AAA.
Mwisho wa maneno katika
mshororo wa kwanza mpaka wa tatu, vina vya kati na vya mwisho vinalingana.
Ambapo kina cha kati kwa mishororo yote ni [e] na kwa vina vya mwisho ni [tu].
Ubeti huu kutoka shairi la" Nia yangu sigeuzi"
uliotungwa na Mohamed Seif Khatib unaonyesha sifa za kimuundo za ushairi kwa
kuwa na idadi maalum ya mistari (mitatu), urari unaokaribiana wa mizani, na
mpangilio maalum wa vina vya nje (AAA). Hii inathibitisha jinsi washairi
wanavyotumia muundo kama sehemu muhimu ya sanaa yao ya lugha.
Muundo huu si tu unaleta
urembo wa kimuziki katika ushairi, bali pia unaweza kusaidia katika kuongoza
mawazo na hisia, na kufanya shairi likumbukike kwa urahisi.
Kwa ujumla: Ni dhahiri kuwa sifa bainifu za ushairi si tu
kanuni za kifundi, bali ni vigezo muhimu vinavyotofautisha ushairi na aina
nyingine za fasihi. Uelewa wa sifa hizi ni muhimu kwa wasomaji, wanafunzi, na
watafiti wa fasihi ili kufahamu na kuthamini kikamilifu utajiri na uzuri wa
ushairi wa Kiswahili.
Hata hivyo, ni muhimu kukiri kuwa
uwanja wa ushairi unaendelea kukua na kubadilika, na hivyo kuleta changamoto
mpya katika ufafanuzi wa sifa zake. Tafiti zaidi zinaweza kufanywa kuchunguza
mabadiliko haya na jinsi yanavyoathiri uelewa wetu wa ushairi wa Kiswahili
katika karne ya 21.
MAREJELEO
Finnegan, R. (2012). Oral Literature in Africa. : Open Book
Publishers.
Hobsbaum, P. (1996). Metre, Rhythm and Verse Form. London:
Routledge
Kipury, S. N. (1983). Oral
Literature of the Maasai. Nairobi: East African Educational Publishers.
Massamba, D. P. B. (2004). Kamusi Elekezi ya Fasihi. Dar es
Salaam: Taasisi ya Taaluma za Kiswahili.
Mulokozi, M. M., & Sengo, T. S. Y. (1995). Historia ya
Fasihi ya Kiswahili. Dar es Salaam: Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Senkoro, F. E. M. K. (2011).
Fasihi Simulizi na Andishi. Dar es Salaam: Mkuki na Nyota Publishers.
Wamitila, K. W. (2002). Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi:
Focus Publishers.
0 maoni:
Post a Comment