18 Jun 2025

 Imeandaliwa na Mtila Mswahili.


UTANGULIZI

Kwa mujibu wa Omolewa (2007) elimu ya jadi ni mchakato endelevu wa mafunzo kupitia maisha ya kila siku, ambapo jamii inawajibika kumfundisha mtoto maadili, ujuzi na mila kwa lengo la kumwezesha kuishi kwa mafanikio ndani ya jamii yake.

Pia Wane (2021) anafafanua kuwa thieta za kijadi ni sanaa ya mawasiliano ambayo huunganisha maonyesho ya uigizaji, nyimbo, ngoma, na mazungumzo kama njia ya kujifunza na kuendeleza maarifa ya jamii.

Aidha, Chikoko (2022) anafafanua thieta za kijadi kama njia ya kuelezea matukio au masuala ya kijamii kwa kutumia vipengele vya sanaa ya utendaji kama sehemu ya elimu isiyo rasmi kwa wanajamii.

Kwa ujumla, thieta za kijadi ni aina ya elimu isiyo rasmi iliyotolewa kwa njia ya vitendo, mazungumzo, maonyesho, na kushiriki katika shughuli za kijamii, ambayo ililenga uendelezaji wa jamii kupitia maadili, ujuzi, na maarifa. Thieta za kijadi ni mfumo wa elimu usio wa kiformali uliokuwepo katika jamii za Kiafrika kabla ya kuanzishwa kwa shule rasmi na mfumo wa elimu ya Magharibi uliokuja na ukoloni. Thieta hizi zililenga kuandaa mtu kuwa mshiriki mzuri wa jamii, mwenye maadili, ujuzi, na maarifa ya kijamii.

Kabla ya ujio wa ukoloni, jamii nyingi za Kiafrika zilikuwa na utamaduni tajiri wa sanaa za maonyesho, ikiwemo sanaa ya thieta za kijadi. Thieta hizi zilihusisha maonesho ya jukwaani yaliyofanyika katika mazingira ya asili au mikusanyiko ya kijamii kwa lengo la kuelimisha, kuburudisha, kukuza maadili na kuendeleza urithi wa jamii.

Thieta za kijadi hazikuhusiana tu na burudani bali pia zilikuwa njia muhimu ya mawasiliano, mafunzo na utatuzi wa migogoro. Katika jamii ya Kiafrika, thieta haikuhitaji jukwaa rasmi wala tamthilia zilizoandikwa; bali ilitumia uigizaji wa moja kwa moja, nyimbo, ngoma, methali, hadithi na maigizo ya maisha halisi. Zifuatazo ni badhi ya thieta za kijadi zilizokuwa zikifanyika kabla ya ukoloni: -

Sherehe za maisha: Thieta hizi zilitolewa kupitia sherehe za kijadi kama vile tohara, ubalehe, ndoa, na mazishi, ambazo zilifundisha vijana kuhusu majukumu yao ya kijinsia, maadili, nidhamu, na utamaduni wa jamii yao. Mfano, kwa jamii ya Wamakonde, wavulana walipitishwa kwenye tohara (likumbi) ambako walijifunza kuhusu uongozi wa familia, heshima kwa wazee, na namna ya kuwa wanaume wa kweli. Wakati wa tohara, walikaa kambini kwa siku kadhaa wakipewa mafunzo ya maisha, kazi, na tabia njema. Kwa Wasambaa, wasichana waliandaliwa kwa maisha ya ndoa kwa kufundishwa namna ya kutunza familia, kupika, na kusimamia kaya. Sherehe hizi hazikuwa tu ibada bali zilikuwa shule za maadili, uongozi, na utambulisho wa kijamii.

Simulizi na hadithi: Hii ilikuwa mojawapo ya theita mashuhuri ambapo wazee walitumia hadithi kufundisha watoto kuhusu maadili, hila, haki, na hekima. Hadithi hizi mara nyingi zilihusisha wanyama kama wahusika. Mfano, hadithi za Sungura na Fisi zilifundisha kuhusu ujanja na matokeo ya tamaa. Sungura aliye mjanja huwakwepa maadui zake kwa kutumia akili badala ya nguvu. Watoto walijifunza kuwa wajanja na wasioonea wengine.
Hadithi hizi zilisimuliwa jioni na zilifuatana na maswali kwa watoto ili kuthibitisha walichojifunza. Kwa hiyo, simulizi zilijenga uelewa wa kijamii, mawasiliano, na maarifa ya maisha.

Nyimbo na mashairi ya kijadi: Nyimbo zilikuwa chombo cha kufundisha maadili, historia ya jamii, na kazi mbalimbali za kijamii. Mashairi yalitumika kueleza hali za maisha, kutoa nasaha, na kusherehekea matukio muhimu. Mfano, kwa Wazaramo, nyimbo za mavuno kama “Lolea lolea twavuna mpunga” zilifundisha mshikamano wa jamii, kazi ya pamoja, na umuhimu wa ardhi. Katika nyimbo za harusi, wasichana walifundishwa kuhusu wajibu wao katika ndoa kupitia mashairi yenye mafundisho kama vile: "Usipoamka mapema, chakula kitachomwa, mume atakukasirikia, ndoa itavunjika.” Nyimbo hizo zilikuwa darasa la wazi lenye mchanganyiko wa burudani na mafunzo.

Kazi za kijamii na mafunzo kwa vitendo: Elimu ya jadi ilitolewa kupitia kazi za kila siku ambapo watoto walijifunza kutoka kwa wazazi na jamii kwa kushiriki moja kwa moja. Mfano ni mtoto wa Wanyakyusa alijifunza kulima kwa kushiriki katika shamba la familia. Alijifunza kupanda, kuvuna, na kuhifadhi mazao. Msichana alifundishwa kupika, kusuka vikapu, na kushona kupitia kushiriki na mama na bibi katika kazi hizo. Elimu hii ilijikita katika vitendo, na ilikuwa ya moja kwa moja, ikiimarisha ujuzi wa maisha na uzalishaji.

Michezo ya kiasili: Michezo ilitumika kufundisha nidhamu, ushirikiano, kujiamini, na kuhimili changamoto. Michezo pia ilichangia maendeleo ya akili na mwili. Mfano, Mchezo wa bao la kete ulifundisha kupanga mikakati, kuhesabu, na subira. Pia, kombolela na michezo ya mbio ziliwafundisha watoto kufanya kazi kwa timu, uvumilivu, na ujasiri. Michezo ilichukuliwa kama fursa ya kujifunza kwa njia ya furaha na kushirikiana.

Baraza la wazee na maamuzi ya kijamii: Baraza la wazee lilikuwa chombo cha maamuzi lakini pia kilitumika kama shule ya elimu ya jamii, hasa kwa vijana waliotakiwa kujifunza kuhusu sheria za kijadi, uongozi, na namna ya kushughulikia migogoro. Mfano, kwa Wairaqw, vijana waliambiwa wahudhurie vikao vya baraza ili kusikiliza mijadala na uamuzi wa wazee kuhusu masuala ya ardhi, ndoa, au migogoro ya familia. Kupitia hayo, walijifunza kusuluhisha kwa amani, kuheshimu mamlaka, na kutambua nafasi ya kila mtu katika jamii.

Matambiko na imani za jadi: Elimu ya kijadi pia ilitolewa kupitia matambiko yaliyofanyika kuomba mvua, kuondoa mikosi, au kusherehekea mavuno. Hii iliwafundisha vijana kuhusu imani, mazingira, na heshima kwa waliokufa. Mfano, kwa Wagogo, kabla ya mavuno walifanya tambiko kwa mizimu kuomba mvua, ambapo walifundishwa kuhusu umuhimu wa mazingira na ardhi katika maisha ya jamii. Katika tambiko la matanga, vijana walielekezwa kuhusu heshima kwa wazazi waliokufa na maana ya mshikamano wa ukoo.

Hitimisho
Thieta za kijadi kabla ya ukoloni zilikuwa mfumo wa kina na mpana wa elimu uliolenga kukuza maadili, ujuzi, na mshikamano wa kijamii.
Kupitia sherehe za maisha, hadithi, nyimbo, kazi za kijamii, michezo, baraza la wazee na matambiko, jamii ziliweza kuwalea watoto kuwa watu wazima wenye maarifa, staha, na uwezo wa kuchangia maendeleo ya jamii. Ingawa mfumo huu haukuwa rasmi kama shule za leo, ulitoa msingi madhubuti wa maisha ya kijamii na kiutamaduni.

 

MAREJEO

Chikoko, V. (2022). Mifumo ya maarifa ya asili na mchango wake katika elimu kwa

maendeleo endelevu barani Afrika. Jarida la Utafiti wa Kielimu Barani Afrika, 10(1), 1–10. https://doi.org/10.30918/AERJ.101.21.092.

Omolewa, M. (2007). Mbinu za jadi za elimu barani Afrika: Umuhimu wake katika dunia

ya sasa. Mapitio ya Kimataifa ya Elimu, 53(5-6), 593–612.

https://doi.org/10.1007/s11159-007-9060-1.

Wane, N. N. (2021). Maarifa ya jadi ya Kiafrika na elimu: Upatanisho kati ya yaliyopita na

ya sasa. Jarida la Kimataifa la Utafiti wa Mwamko wa Kiafrika, 16(1), 34–50. https://doi.org/10.1080/18186874.2021.1902748.

 

0 maoni:

Post a Comment

Powered by Blogger.

Wasiliana nami papo kwa papo

Name

Email *

Message *

Ads 468x60px

Breaking News

Top Featured

Featured Posts

Sample text

Sample Text

Recomended

Facebook

Advertise

Most Popular

Connect With Us

Followers

Social Icons

Pages

Pages

BTricks

Pages

Popular posts

Tafuta chochote ukiwa hapahapa

Kategori

Recent Comments

You can replace this text by going to "Layout" and then "Page Elements" section. Edit " About "

recent posts

Video Of Day

TRANSLATE

Instructions

Video

Flickr Images

FURAHIA UWEPO WAKO HAPA

Logo Design by FlamingText.com
Logo Design by FlamingText.com

Imetembelewa mara

NUMBER OF VIEWERS

Popular Posts

SAJIRI

Definition List

premium-wordpress-themes.org